×

Pasi ya Ajibu yamkuna Samatta, Atuma Salamu

STORI: Na Wilbert Molandi na Said Ally | CHAMPIONI

PASI ya bao la dakika ya 68 iliyopigwa na Ibrahim Ajibu imemkuna mshambuliaji wa Klabu ya K.R.C Genk ya Ubelgiji, Mbwana Samatta. Ajibu alipiga pasi hiyo maarufu kwa jina la ‘outer’ kwenye mechi ya Ligi Kuu Bara iliyowakutanisha na Prisons mechi ambayo ilimalizika kwa Simba kushinda mabao 3-0 Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Pasi hiyo aliyopiga Ajibu ilizaa bao baada ya mshambuliaji wa timu hiyo, Laudit Mavugo, kufunga kwa kichwa kwenye dakika ya 68 ya mchezo huo. Hiyo ni ishara tosha kwa mshambuliaji huyo kuonekana akifuatilia ligi kuu ya Bongo baada ya kuiona pasi hiyo ya bao.

Samatta, juzi usiku alishindwa kujizuia na kuficha hisia zake na kutwiti kwenye akaunti yake ya Twitter akisema: “Ibrahim Ajibu mtoto nyo…** sana wewe, umepiga pasi ya kiwango cha kimataifa.”

Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Tanzania, juzi Ijumaa alirejea uwanjani na kuifungia KRC Genk bao la pili katika ushindi wa 3-0 dhidi ya mahasimu, SintTruiden katika mchezo wa Ligi Kuu ya Ubelgiji, Uwanja wa Stayen, Sint-Truiden, St.-Trond.