The House of Favourite Newspapers

Niyonzima, Haji Wataja Kilichoiponza Yanga SC

STORI: Wilbert Molandi na Ibrahim Mussa | CHAMPIONI

KIUNGO Haruna Niyonzima na beki Haji Mwinyi, wametaja sababu zilizoifanya timu yao ya Yanga itupwe nje ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na timu ya Zanaco ya Zambia. Yanga imeondolewa katika michuano hiyo kwa hasara ya kukosa bao la ugenini kufuatia sare ya bao 1-1 kabla ya juzi kutoka 0-0 katika mchezo wa marudiano uliopigwa Zambia kwenye Uwanja wa Mashujaa.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Mwinyi alisema sababu kubwa ni kushindwa kulinda ushindi wao katika mchezo wa nyumbani. “Kiukweli kwetu ni maumivu kwa sababu malengo yetu msimu huu katika Ligi ya Mabingwa yalikuwa ni kufika nusu fainali lakini tumetolewa kwa faida ya bao la ugenini maana muda wote tulicheza kwa kujituma ili tupate bao lakini ilishindikana.

“Nadhani haikuwa bahati yetu kusonga mbele, binafsi naona kilichosababisha hadi tukaondolewa ni kutoweza kulinda ushindi wetu katika mchezo wa awali hapa nyumbani tofauti na wenzetu walivyofanya kwao licha ya sare ya bila kufungana,” alisema Mwinyi.

Kwa upande wake Niyonzima ambaye pia ni nahodha wa timu hiyo, alisema idadi kubwa ya majeruhi kwenye kikosi chao ndiyo ilisababisha waondolewe kwenye michuano hiyo. “Katika timu wanapokosekana wachezaji wawili hadi watatu ni pengo kubwa, kama ilivyokuwa kwetu, tulimkosa (Donald) Ngoma na (Amissi) Tambwe katika mechi hii kutokana na majeraha, lakini pia viungo (Thabani) Kamusoko na (Justin) Zulu walicheza wakiwa bado hawajapona vizuri majeraha yao,” alisema Niyonzima.

 

Comments are closed.