×

TFF Yashusha Presha ya Pointi tisa Simba SC

Sweetbert Lukonge | CHAMPIONI| Dar es Salaam

SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limewataka viongozi wa Simba kutokuwa na wasiwasi na waamuzi watakaochezesha mechi zao zote tatu za Ligi Kuu Bara huko Kanda ya Ziwa.

Timu ya Simba hivi sasa ipo mkoani Kagera ikisubiri kucheza na Kagera Sugar, Jumatatu kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba, baada ya hapo itasafiri kwenda Mwanza kupambana na Mbao FC pamoja na Toto Africans.

TFF imefikia uamuzi huo baada ya baadhi ya viongozi wa Simba kulalamika wakitaka wapangiwe waamuzi wazuri wenye uwezo mkubwa wa kuzitafsiri sheria 17 za soka.

Akizungumza na Championi Jumatano, Mwenyekiti wa Kamati ya Waamuzi ya TFF, Salum Chama, alisema kuwa Simba hawana haja ya kuwa na wasiwasi na waamuzi wanachotakiwa ni kujipanga kwa ajili ya kuhakikisha wanafanya vizuri kwenye mechi zao hizo.

Alisema waamuzi wote watakaochezesha mechi hizo ni wazuri na wana uwezo mkubwa wa kuzitafsiri sheria hizo 17 za soka na kutoa maamuzi sahihi yasiyokuwa na upendeleo kwa timu yoyote ile.

“Kuna malalamiko ya hapa na pale ambayo tumekuwa tukiyasikia kutoka kwa baadhi ya viongozi wa Simba kuhusiana na waamuzi watakaochezesha mechi zao za Kanda ya Ziwa.

“Niwaombe tu kutokuwa na wasiwasi kwani waamuzi wote watakaochezesha mechi zao tunawaamini na wapo vizuri katika kuzitafsiri sheria zote 17 na kutoa maamuzi sahihi, hivyo wao wajiandae tu,” alisema Chama.