
KIUNGO mpya wa Azam FC, Salmin Hoza aliyejiunga na timu hiyo hivi karibuni akitokea Mbao FC ya Mwanza, ameamua kumalizana na mabosi wa Yanga baada ya kuwarudishia fedha zao shilingi milioni tano alizochukua kama ‘kishika uchumba’ wakati timu hiyo ilipokuwa ikihitaji saini yake kabla ya kutua Azam FC.
Ishu ilikuwa hivi, Yanga ndiyo ilikuwa timu ya kwanza kuhitaji saini ya Hoza na kumpa kiasi cha shilingi milioni 5 kwa ajili ya kumtuliza asisaini timu nyingine huku wakimpa mkataba wa makubaliano lakini dili hilo lilikuja kuvunjwa na Azam ambao waliamua kupanda dau na kumsainisha kwa mkataba wa miaka miwili.
Baada ya kiungo huyo kuona amesaini timu mbili ambapo ni kinyume kwa mujibu wa sheria za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kusaini timu mbili kwa wakati mmoja akaamua kujiongeza na kuwarudishia fedha mabosi hao wa Yanga.
Akizungumza kupitia Kipindi cha Spoti Hausi kinachorushwa na GlobalTv Online, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Habari cha Yanga, Godlisten Anderson ‘Chicharito’ amesema Hoza alirudisha fedha hizo ambazo walimpa pamoja na kuomba radhi kwa kitendo ambacho alikifanya.
“Unajua yule Hoza sisi ndiyo tulikuwa wa kwanza kumfuata kwa nia ya kumsajili kwa msimu ujao lakini walichofanya Azam ni kwenda kwa wazazi wake na kuongea naye na kwa kuzingatia masuala ya familia akashindwa kukataa ndiyo maana akatua kwao licha ya kuwa sisi ndiyo tulianza kumfuata na kumpa fedha za kumsajili.
“Lakini kwa ajili ya kuzima ishu nzima ya kusajili timu mbili, yeye (Hoza) alituma barua ya kuomba msamaha kwetu kwa kilichotokea pamoja na kuturudishia zile fedha ambazo tulimpa mwanzoni.
“Ila kumkosa kwake kwetu siyo pigo kubwa kwani kwenye listi yeye alikuwa chaguo la tatu kusajiliwa hivyo tumebakiwa na nafasi mbili ambazo tutazifanyia kazi,” alisema Chicharito.