
Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es salaam limewakamata vinara wa wizi wanaotumia Pikipiki kuwaibia akina mama na watalii wawapo kwenye ufukwe wa Coco Beach pamoja na wengine wanaotumia magari kufanya uhalifu wa aina hiyo barabarani.
Akitoa taarifa hiyo, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dar, Lucas Mkondya amesema kuwa wamekamatwa watuhumiwa 10 wa uhalifu huo, vinara wanne ambao ndio viongozi wa makundi yanayoba kwa njia hiyo pamoja na wengine 13 ambao waliongezeka baada ya wenzao kuwabana na kutajwa hivyo kufikisha idadi ya waarifu 23.
Kamanda huyo aliwataja Vinara hao ambao wanatajwa kuwa viongozi kuwa ni Carlos Tobiasi (18), Boniface George (20) , Hakida Twaha (21) na Deogratius Byamuya (26) wote wakiwa ni wakazi wa Kimara jijini Dar es salaam.
“Tumefanikiwa kuwabana wahusika hawa wamewataja wenzao wote na mahala wanapohifadhi mali zao ambapo tumekamata Televisheni Moja , Laptop 3 na simu za mkonini,” alisema Kamanda.
Kamanda amemalizia kwa kusema kuwa watuhumiwa watafikishwa mahakamani na kuwahonywa wale wote wenye tabia ya kununua mali za wizi kwani watuhumiwa wamewataja kwa majina wale wote waliowauzia.
“Tunampango wa kuwakamata na tutawafungulia kesi mahakamani kwa kununua mali za wizi kwani tumeshawabaini kwasababu wametajwa kwa majina yapo na tunayo hapa,” alisema Kamanda.