




MZEE Juma Waziri Juma ambaye aliwahi kuwa mkuu wa mikoa mbalimbali nchini enzi za utawala wa Mwalimu Julius Nyerere, amemwangukia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, kwa kumtaka aingilie kati kufuatia nyumba yao kutapeliwa na mtu mmoja aitwaye Mpango waliyedai kuwa naye alimuuzia raia wa China ambaye alikuwa mpangaji wa nyumba yake.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, mtoto wa mzee huyo aitwaye Maida Waziri amesema kuwa nyumba yao imetapeliwa na mpangaji wao aliyekuwa amepangishwa kwa kipindi cha zaidi ya miaka kumi na baada ya mkataba wa malipo ulipoisha alitakiwa kulipia pango lingine lakini alikaidi akidai kuwa nyumba ni ya kwake na kwamba aliuziwa.
Amesema kuwa kabla ya mpangaji huyo kuuziwa nyumba na watu wasiojulikana, familia hiyo ilipata taarifa kwamba nyumba ilitaka kuuzwa na fedha zingepita benki ya Twiga Bancorp, hatua iliyowalazimu kupeleka zuio lakini benki hiyo haikufuata maelekezo hayo.
Maida amefafanua kwamba baba yake amekuwa mtumishi wa umma kwa takribani zaidi ya miaka 30 na alijenga nyumba zake wakati akiwa mtumishi wa serikali enzi hizo.