
Kituo Cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) leo Aprili 25, 2018 kimezindua ripoti maalum ya Haki za Binadamu ya mwaka 2017 juu ya matokeo na mapendekezo muhimu kutokana na mambo mbalimbali yanayolihusu Taifa na wananchi wake.

Katika uzinduzi wa ripoti hiyo, baadhi ya mambo yaliyotajwa ni matukio makubwa yaliyoathiri au kuimarisha ulinzi wa haki za binadamu kwa mwaka 2017.

Akiwasilisha baadhi ya mambo yaliyomo ndani ya ripoti hiyo, Ofisa Utafiti wa kituo hicho, Fundikila Wazambi amesema taarifa ya ripoti hiyo inaonyesha mwanamuziki Ibrahim Mussa ‘Roma Mkatoriki’ na wenzake waliripotiwa kutekwa na kuteswa na ‘watu wasiojulikana’ na zuio la mikutano ya kisiasa kwa wanasiasa nje ya majimbo yao.

Aidha, ripoti hiyo imezungumzia tukio la aliyekuwa Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) na Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu (mbunge wa Singida Mashariki) aliyeshambuliwa kwa risasi na ‘watu wasiujulikana’ nje ya makazi yake mjini Dodoma, Septemba, mwaka jana.

Pamoja na mambo mengine, ripoti hiyo pia imezungumzia matukio ya utekaji, mauaji na kutoweka katika mazingira ya kutatanisha kwa mwandishi wa habari, Azory Gwanda ambaye mapaka sasa hajulikani alipo.