
KAMPUNI ya Global Publishers inayochapisha Magazeti ya Risasi, Uwazi, Championi, Amani, Ijumaa na Spoti Xtra, wiki ijayo itatoa zawadi ya tuzo za shukrani kwa wauzaji wa magazeti (mavenda) wapatao 16 ambao walianza na kampuni hiyo tangu mwaka 1998.
Wikiendi iliopita katika Uwanja wa Taifa wa Burudani, Dar Live, uliopo Mbagala Zakhem, Dar, kampuni hiyo iliweza kufanya tamasha maalum la kuwashukuru wauzaji hao sambamba na wasomaji lililotambulika kwa jina la Tamasha la Shukrani ambapo mavenda walijitokeza kwa wingi na kueleza changamoto wanazokutana pamoja na mafanikio.

Mrisho Hamza ambaye ni muuuza magazeti katika kituo cha mabasi yaendayo mikoani Ubungo alifanikiwa kupewa zawadi ya shilingi laki moja na Mkurungezi wa Kampuni ya Global, Eric Shigongo kufuatia kuvutiwa na ushuhuda wake wa kazi ya kuuza magazeti ambayo imemsaidia kujenga nyumba mbili.
“Nimeanza kuuza magazeti tangu mwaka 1999 na kufanikiwa kujenga nyumba mbili, moja ipo Mbezi
Maramba Mawili ina vyumba viwili na nyingine Kibaha, sina shida, magazeti haya ya Global yamenisaidia sana,” alisema.
Akizungumza na umati wa mavenda waliojitokeza, Eric Shigongo aliwashukuru kwa kujitokeza kwao na kuwaambia asiwepo mtu wa kuwadharau kutokana na kufanya kazi hiyo.
“Tumekuja kuwasikiliza, mseme kila kitu kinachowasumbua na maoni yenu tutayafanyia kazi, najua ukweli siku zote unauma lakini haupuuzwi. Sisi ni familia moja na tatizo likitokea ni letu sote,” alisema Shigongo.
Shigongo pia alimuita mmoja wa mavenda anayeuzia magazeti eneo la Namanga, Said Limaga na kutoa ushushuda wake.
“Huyu kijana huwa nakutana naye mara nyingi, amekuwa akinishauri vitu vingi na kuwapelekea wahusika kuyafanyia kazi. Nimeanza naye zamani na namjua vizuri tangu anamsomesha mtoto wake,” alisema Shigongo.
Limaga naye alishukuru kwa kupewa nafasi ya kuzungumza ambapo alisema anashukuru magazeti yameweza kumsaidia kumsomesha binti yake na kufanikiwa kupata daraja la kwanza katika masomo ya sayansi.
“Mwanangu Aziza Limaga alikuwa akisoma Shule ya Sekondari, Tabora Girls na amefaulu na sasa yupo JKT akijiandaa kuingia chuo,” alisema Limaga.
Kutokana na ushuhuda huo, Shigongo aliahidi kumzawadia Limaga shilingi laki tano ili ampatie Aziza anunue chochote kama sehemu ya zawadi yake kwa kufaulu vizuri na iwe kumbukumbu kwake.
“Amemsomesha mwanaye mpaka amefaulu kwenda chuo kwa kazi hiihii ya magazeti, kila nikikutana naye nilikuwa namtia moyo kama anaweza na kumuomba Mungu katika mambo yake,” alisema Shigongo.
Shigongo alimaliza kwa kuwaita mbele, mavenda ambao walikuwa jumla ya 16, waliokuwa pamoja tangu kuanzishwa kwa biashara ya Magazeti ya Global mwaka 1998 na kuwaahidi kuwapatia zawadi ya tuzo za shukrani kutokana na mchango wao mkubwa.
https://globalpublishers.co.tz/global-yatoa-shukurani-kwa-wasomaji-magazeti-dar-live