







Bugingo Emmanuel ameibuka mshindi wa shindano la biashara la Kuza Ofisi na FINCA na kuondoka na kiasi cha TZS milioni 10 baada ya shindano la muda wa miezi mitatu na lililokuwa na zaidi ya washiriki elfu moja walioshiriki, ni washriki wanne ndio waliowasilisha mipango yao ya biashara kwa jopo la majaji na kupigiwa kura na watazamaji.
Akiongea katika onyesho la mwisho la shindano la Kuza Ofisi na FINCA jijini Dar es salaam, Naibu Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira, Mhe. Anthony Mavunde aliipongeza FINCA kwa kutekeleza jitihada za kibunifu kwa ajili ya kusaidia kukuza wajasiriamali wadogo kwa wakati. Alisema kwamba serikali inaendelea kuandaa mazingira mazuri kwaajili ya maendeleo ya biashara nchini. “Ninatoa wito kwa vijana kuchangamkia fursa zinazotolewa na mifuko ya uwezeshaji ya serikali ambayo imetengwa kwaajili ya maendeleo ya biashara.
Vile vile aliipongeza benki ya FINCA Microfinance kwa jitihada zake zenye lengo la kusaidia kukuza wafanyabiashara wadogo SMEs nchini ‘Ninaipongeza FINCA kwa kubuni mipango hii ya kibunifu ambayo sio tu kwamba inasaidia kukuza biashara ndogo ndogo lakini pia inawapatia vijana ujuzi na stadi za biashara alisema Mavunde.
Afisa Uendeshaji Mkuu wa Benki ya FINCA bwana Alfred Vanderlin alisema ‘Benki ya FINCA inaboresha na kurahisisha mchakato wake wa kutoa mikopo na utoaji wa huduma kwa wateja kwaajili ya kupunguza gharama na kuwawezesha wateja kufanya biashara kwa urahisi’.
Aliongeza kuwa, FINCA inaendeleza utamaduni wa ubunifu na uvumbuzi na inaamini kwamba mafanikio ya maisha yajayo katika kupanua upatikanaji wa huduma za kifedha utapatikana kupitia uboreshaji wa teknolojia na utoaji wa huduma bora zenye kiwango cha juu kwa wateja’.
Shindano hili lililodumu kwa muda wa miezi mitatu lilikuwa na lengo la kuwezesha wafanybiashara wadogo kwa kuwapatia stadi za biashara, elimu na kuwapatia mtaji wa kiasi cha thamani ya TZS milioni 10 kwa wazo bora zaidi la biashara litakalowasilishwa. Mshindi wa pili wa shindano hilo bwana Sadiki Hassan aliondika na kiasi cha shilingi milioni 5 wakati mshindi wa tatu wa shindano hilo bwana Reuben Waya aliondoka na shilingi milioni 3.
Shindano la kuza ofisi na FINCA awali lilitekelezwa katika wilaya nne za mkoa wa Dar es salaam ambazo zinajumuisha Kinondoni, Ilala, Temeke na Ubungo. Wilaya hizi ziliambatanishwa katika matawi ya benki ya FINCA ambayo yamewekwa kimkakati katika maeneo ya Tegeta, Ilala, Victoria na katika barabara ya Pugu kuelekea uwanja wa ndege.