The House of Favourite Newspapers

Makonda Asimulia Alivyofukuzwa Nyumba ya Kupanga – Video

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, amefunguka namna alivyofukuzwa kwenye nyumba ya kupanga, kisa hana pesa ya kulipia pango la nyumba hiyo wakati pesa ameitumia katika shughuli za kueneza neno la Mungu huko Moshi, mkoani Kilimanjaro.

 

Makonda amesema hayo usiku wa kuamkia leo Mei 17, 2019 wakati akitoa nasaha kwa vijana wa vyuo mbalimbali waliojumuika kwenye Viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe, Dar,  kumshukuru Mungu na kumsifu kupitia Kongamano la Victory Campus Night 2019 lililoandaliwa na Kanisa la VCCT Mbezi Beach.

 

“Mwaka mmoja wakati nikiwa Chuo cha Ushirika Moshi niliandaa kongamano, rafiki yangu mmoja akaniahidi atanisaidia, lakini dakika za mwisho akanitosa, nilikuwa nimepanga nyumba na mke wangu Sinza-Mori maeneo ya Meeda, nyumbani nilikuwa na pesa ya kulipia pango kwa mwaka, nikamtafuta mwenye nyumba kumuomba kwamba pesa niliyo nayo nitaitumia kwenye huduma, hivyo nitamtafutia pesa ya kodi, lakini alikataa.

 

“Nilimwambia mke wangu anitumie pesa yote akatuma, nikaweka kila kitu sawa nikafanikisha huduma hiyo. Mwenye nyumba akasema ‘nataka pesa yangu’, dalali alitafuta mtu mwinginge wa kumpangisha, akalipia ili nihame kwenye nyumba, siku ya mwisho polisi wakaambiwa sitaki kutoka.

“Asubuhi simu yangu ikaita, mtu mmoja akaniambia nikaonane naye, alinipa shilingi milioni nne, wakati narudi akanipigia simu Mbunge Mwambalasa akaniambia nikutane naye Ubungo Tanesco, akanipa shilingi milioni mbili, nikapigiwa simu tena na rafiki yangu mwingine akaenda kunipa milioni nne, nikawa nimepata milioni saba.

 

“Nikapata nyumba na kununua makochi mapya, lakini yule dada aliyenifukuza hakumaliza siku nyingi akafa, ninaielewa kazi ya msalaba, ukinichezea utaelewa, nasema kwa sababu ninaelewa wala siyo kujitapa.

“Mimi nilikuwa nakwenda kulala kwenye mabenchi, maisha yangu yalikuwa magumu lakini sasa hivi nikipita utajua nimepita, nikiongea utajua nimeongea, sasa wewe unaringia nini hata mwaka wa tatu hujafika wala cheti huna, mimi na cheo changu namtambua Mungu,” amesema Makonda.

MSIKIE AHAPA AKIFUNGUKA

 

 

Comments are closed.