×

Kauli ya Marekani kuhusu Kuondoa Majeshi Yake Iraq

WAZIRI  wa Ulinzi wa Marekani, Mark Esper, amekanusha madai kuwa majeshi yake yanataka kuondoka Iraq baada ya barua kutoka kwa Jenerali wa Marekani kupendekeza waondoke.

Barua ilisema kuwa Marekani itaondoa vikosi vya majeshi yake siku zijazo au wiki baada ya wabunge wa Iraq kuwataka waondoke.

Esper alisema kuwa hakuna maamuzi yeyote ya kuondoka. Mkanganyiko huu wa vitisho ulikuja mara baada ya Jeshi la Marekani kumuua Kamanda wa Jeshi wa Iran, Qasem Soleimani.

Jenerali Soleimani aliuawa katika mapambano ya anga huko Baghdad siku ya Ijumaa baada ya Rais wa Marekani, Donald Trump,  kuamuru wafanye hivyo. Mauaji hayo yameongeza mvutano katika ukanda huo, huku Iran ikitishia kulipiza kisasi.

 

Nini kiliandikwa kwenye barua?

Inaonekana kuwa barua hiyo ilitumwa na Brigedia Jenerali William H Seely, Mkuu wa jeshi la Marekani,  katika kikosi kilichopo Iraq, kwenda kwa mkurugenzi msaidizi wa opereshani ya pamoja Abdul Amir.

Barua ilianza hivi: “Ndugu, kwa heshima ya Jamhuri ya Iraq, na maombi yaliyotolewa na bunge la Iraq, pamoja na waziri mkuu na mkuu wa operesheni za pamoja (Combined Joint Task Force) tutaondoa vikosi vyetu vya jeshi katika siku zijazo au wiki kadhaa ili kujiandaa na hatua nyingine.

 

Iliendelea kusema kuwa hatua kadhaa zitafanyika ikiwa pamoja na kuwa na ndege nyingi angani wakati wa saa za usiku ili kuhakikisha kuwa wanaondoka kwa usalama na utaratibu unaofaa.

Vilevile hatua hii itaondoa mitazamo kuwa labda tuna mpango wa kuongeza majeshi zaidi katika ardhi ya Iaq.


Hatua hii imeelezewa vipi?

Bwana Esper aliwaambia waandishi wa habari nchini Marekani: “Hakuna hatua yeyote iliyofanywa kuhusu majeshi ya Marekani kuondoka Iraq. Sifahamu chochote kuhusu barua hiyo… Tunajaribu kufuatilia kujua barua hiyo imetokea wapi na ina maana gani?

 

“Kiufupi, hatujafanya maamuzi ya kuondoka Iraq.”

Kiongozi wa juu wa jeshi la Marekani, Mark Milley, alisema pia kuwa barua hiyo ilikuwa ya kimakosa.

Kwa sababu ilikuwa imeandikwa vibaya, haikuwekwa sahihi na haikupaswa kutolewa. Ilikuwa ikisambazwa kwa ajili ya kuongeza maelezo, kutoka kwa Wairaq pia.

 

“Barua ilitumwa kwa baadhi ya viongozi wa jeshi la Iraq ili kuweka utaratibu wa usafiri wa anga pamoja na mambo mengine muhimu. Na barua ilitumwa kwao na kuanza kusambazwa kwa watu na sasa imeleta mtazamo wa uhasama.”

Jenerali Milley alirudia pia kusema kuwa jeshi la Marekani haliondoki Iraq.

Nini kilitokea?

Jenerali Milley alisema kuwa suala hilo linafanyiwa kazi na Iraq lakini hakutoa ufafanuzi zaidi.

Mwandishi wa shirika la habari la Uingereza (BBC), Jonathan Beale, alisema kuwa alitaarifiwa kuwa barua hiyo ilitaka Iraq kufahamu kuwa jeshi la Marekani linaondoka katika himaya ya ‘Green Zone’ na kwenda kutoa huduma ya ulinzi maeneo mengine.

 

Majeshi ya Marekani na nchi nyingine yanafanya nini Iraq?

Kuna zaidi ya wanajeshi 5,000 wa Marekani  nchini Iraq ikiwa sehemu ya ushirikiano wa operesheni ya pamoja iliyoanzishwa mwaka 2014 kupambana dhidi ya kundi la kigaidi la lslamic State ambalo limevamia sehemu kubwa ya Syria na Iraq.

 

Kuna raia kadhaa wa Marekani katika nchi hiyo ambao wanasaidia kutoa huduma mbalimbali.

Vilevile lengo kuu la majeshi hayo ni kutoa mafunzo ya kijeshi na kuboresha jeshi la Iraq kwa vifaa.  Jumapili iliyopita, wabunge walipiga kura na kufikia maamuzi kuwa jeshi hilo liondoke mara baada ya mauaji ya Jenerali Soleimani.

 

Rais Trump alitoa vitisho kadhaa kwa Iraq kuwa kama majeshi ya Marekani yataondolewa kwa nguvu basi wategemee kiama, au njia rahisi ni Iraq wawalipe kiasi chote cha fedha walichotumia kuwekeza katika nchi hiyo ambazo ni mabilioni ya fedha.

 

Leave a Comment