The House of Favourite Newspapers

Sh Mil 30, Kichuya Mali ya Yanga

0

WINGA wa zamani wa Simba, Shiza Kichuya, amekubali kusaini mkataba wa kukipiga Yanga katika usajili wa dirisha dogo msimu huu wa Ligi Kuu Bara.

 

Kichuya hivi sasa anakipiga katika Klabu ya Pharco inayoshiriki Ligi Daraja la Pili nchini Misri aliyojiunga nayo mwaka jana mara baada ya kumalizana na Simba iliyokuwa inammiliki.

 

Pharco ilimnunua Kichuya kutoka Simba kwa dau la Sh milioni 196 kabla ya kumtoa kwa mkopo ENPPI inayoshiriki ligi kuu ya nchini humo kwa ajili ya kumuongezea uzoefu zaidi.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatatu, viongozi wa Yanga hivi sasa wapo kwenye mazungumzo ya kukamilisha usajili wa winga huyo aliyeomba dau la Sh 30mil kwa mkataba wa miezi sita pekee kwa mkopo.

 

Mtoa taarifa huyo alisema bado mazungumzo yanaendelea kati ya winga huyo na viongozi ambao wenyewe wanamtaka apunguze dau hilo ambalo ni kubwa, haliendani na muda wa mkataba ambao ni mdogo.

 

Aliongeza kuwa kama Kichuya akikubali kupunguza dau hilo, basi haraka viongozi watampa mkataba winga huyo mwenye kasi na uwezo mkubwa wa kupiga krosi na kona.

 

“Kichuya ni yeye mwenyewe anajichelewesha kusaini mkataba wa kuichezea Yanga, kwani kila kitu kimekamilika baada ya kupokea ofa yake anayoitaka kabla ya kumtaka kupunguza.

 

“Amekubali kujiunga na Yanga katika usajili huu wa dirisha dogo kwa mkataba wa miezi sita kwa mkopo lakini tatizo lililopo ni kuwa kiwango cha fedha ambacho amekitaka ni kikubwa, hakiendani na muda wa mkataba aliouomba asaini.

 

“Yanga walikuwa tayari kumpa kiwango hicho cha fedha anachokitaka lakini muda wa mkataba uwe mrefu kwa maana ya miaka miwili na siyo miezi sita kama anavyotaka yeye,”alisema mtoa taarifa huyo.

 

Alipotafuta Mkurugenzi Uwekezaji wa Kampuni ya GSM Hersi Said anayewezesha kutoa fedha katika usajili wa Yanga, alisema: “Kila kitu kuhusiana na usajili kipo kwenye benchi la ufundi na sisi kama kampuni tunawezesha katika kutoa pesa.”

 

Sweetbert Lukonge, Dar es Salaam

Leave A Reply