MAPEMA leo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu upande wa utetezi katika kesi inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa Tanzania(MSD), Lauren Bwanakunu na mwenzake, wameutaka upande wa mashtaka iwaeleze tarehe ijayo upelelezi umefikia wapi.
Hatua hiyo imekuja baada ya Wakili wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru), Fatima Waziri, kuieleza mahakama kuwa uchunguzi wa shauri hilo unaendelea na upo kwenye hatua nziri.
Ndipo wakili wa utetezi, Oscar Magolosa, alidai kuwa upande wa mashtaka wawaeleze upelelezi umefikia wapi kwa kuwa kila wanapokuja mahakamani hapo wamekuwa wakija na kauli hiyo.
Katika kesi hiyo mshtakiwa mwingine ni Byekwaso Tabura ambapo wote kwa pamoja wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 46/2020.
Baada ya maelezo hayo Hakimu Mkazi Mkuu, Janeth Mtega, ameahirisha shauri hilo hadi Septemba 7, mwaka huu litakapokuja kwa ajili ya kutajwa.
Katika kesi ya msingi washtakiwa hao wanadaiwa kati ya Julai Mosi, 2016 na Juni 30, 2019, katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam na maeneo mbalimbali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa makusudi washtakiwa waliongoza genge la uharifu, na shtaka la pili ni kuisababishia hasara MSD, tendo wanalodaiwa kulitenda kati ya Julai Mosi, 2016 na Juni 30, 2019, katika eneo la MSD ambapo washtakiwa waliisababishia MSD hasara ya Sh 3.8bilioni.
Katika shtaka lingine la matumizi mabaya ya madaraka linalomkabili Bwanakunu, inadaiwa kati ya Julai Mosi, 2016 na Juni 30, 2019 katika Ofisi za MSD zilizopo Keko, kwa makusudi alikiuka sheria ya umma kwa kutumia madaraka yake vibaya kwa kuwaongezea nyongeza ya mishahara na posho wafanyakazi wa MSD, bila kibali cha Katibu Mkuu Utumishi na hivyo kuisababishia hasara mamlaka hiyo kiasi cha Sh. bilioni 3.
Washtakiwa hao wanadaiwa kati ya Julai Mosi, 2016 na Juni 30, 2019 katika Ofisi za MSD zilizopo Keko, walishindwa kutunza vifaa tiba na dawa vilivyopo MSD visiharibike na matokeo yake, vifaa hivyo viliharibika na kuisababishia hasara MSD ya Sh. milioni 885.

