Chadema Iringa Yalia na Hujuma za ‘Wasiojulikana’
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Mkoa wa Iringa kimelia na hujuma zinazofanywa na watu wasiojulikana kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 28 mwaka huu.
Akizungumza na wanahabari leo, Mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Iringa, William Mungai, amesema miongoni mwa hujuma wanazofanyiwa wagombea wao ni pamoja na kuvamiwa njiani, kupigwa na kunyang’nywa fomu wanapokuwa wakizirudisha.
Katika matukio hayo, Mungai alisema hivi karibuni mgombea Ubunge wa Jimbo la Kilolo akiwa anaingia amekaribia ofisi ya Halmashauri ya Wilaya hiyo kurudisha fomu alivamiwa na vijana watatu ambao walimshambulia na kutaka kumnyang’anya fomu hizo.
Mungai alisema, hata hivyo, mgombea huyo kwa kushirikiana na wanachama wa chama hicho waliokuwa eneo hilo walishirikiana na kumwokoa mgombea huyo na kuziokoa fomu hizo.
Kufuatia matukio hayo, Mungai ameliomba jeshi la polisi mkoani humo kuwasaidia kuwasaka wahalifu hao ili sheria iweze kufuata mkondo wake na kufanyika uchaguzi wa salama na amani.
HABARI/PICHA NA WAANDISHI WETU