MGOMBEA urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. John Magufuli, amesema serikali yake haibagui aina ya nyumba katika kuwaunganishia wananchi umeme, hata nyumba iwe ya nyasi.
Amesema hayo akiwa katika mwendelezo wa kampeni zake alipokuwa Igalula (Tabora) njiani kuelekea Itigi (Singida).
”Tunapeleka umeme hata kwenye nyumba za majani sawa, lakini tungependa zaidi tupeleke umeme kwenye nyumba za bati na hiyo ndiyo Tanzania ninayotaka kuijenga,” amesema Magufuli.
Aidha Magufuli amewataka wananchi kujitahidi na kutamani zaidi kujenga nyumba za bati na zenye ubora kwa kujiwekea malengo na akiba kwa kipindi husika pasipo kuogopa bei za zana za ujenzi ama kusikiliza maneno ya watu.
”Ukipata hela yako jenga nyumba nzuri, nataka niwaeleze hilo hata ukipata Sh 10,000 nenda kanunue bati, chukua matofali yako anza kuyafyatua; maudongo yapo tena udongo mzuri tu siyo lazima ufyatue matofali ya ‘block’,” amesema.
