WATU watano wamefariki dunia na wengine 10 wamejeruhiwa vibaya katika ajali ya barabarani iliyohusisha daladala na lori la mchanga katika eneo la Chang’ombe jijini Dar es Salaam iliyotokea alfajiri ya leo Jumatatu, Oktoba 5, 2020.
Kamanda wa Polisi Temeke jijini Dar es Salaam, Amon Kakwale, na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, wamethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kwamba jeshi hilo linaendelea na uchunguzi kuhusu chanzo cha ajali hiyo.
Kamanda wa polisi kanda maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema waliokufa ni pamoja na wanaume watatu na wanawake wawili waliokufa papo hapo.
Kwa mujibu wa Kamanda Mambosasa, chanjo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva wa basi hilo kwa kushindwa kuzingatia taa za barabarani.
Kwa mujibu wa mashuhuda, ambao wengine walikuwa sehemu ya abiria kwenye basi hilo lililokuwa linatoka Temeke kwenda Muhimbili, wamesema pamoja na kumsisitiza dereva kuzingatia alama hizo, alipuuza kabla ya basi hilo kugongana na lori kwenye makutano.
Daktari Meshack Shimwela, Mganga Mkuu Hospitali ya Rufaa ya Temeke amesema kuwa wengine wanne waliojeruhiwa walipata huduma ya kwanza na tayari wamepelekwa hospitali ya Muhimbili kwa tiba zaidi huku wengine wakiendelea kupata matibabu katika hospitali ya Temeke.
View this post on Instagram




