
TUME ya taifa ya uchaguzi nchini Uganda imelipelekwa daftari la wapiga kura Uholanzi kwa ajili ya kuhakikiwa kuelekea kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika mwezi Januari 2021.
Katika hatua hiyo tume imeipa zabuni kampuni ya Uholanzi kuondoa majina ya watu walioandikishwa zaidi ya mara moja kabla ya uchaguzi kuanza.
“Tumeanza mchakato wa kuwathibitisha wapiga kura ili kuhakikisha wanaostahili tu wanaonekana kwenye daftari na kwamba watapiga kura mara moja,” msemaji wa tume hiyo, Paul Bukenya, amenukuliwa akisema.
Hata hivyo, bado haijulikani kama vyama vya siasa vilijulishwa kuhusu hatua hiyo.
Wananchi wa Uganda watapiga kura kuchagua rais na wabunge Januari 14, 2021 ambapo wagombea wa urais ni 11 akiwemo Rais Yoweri Museveni.