
UMOJA wa Mabalozi wa Afrika leo wametembelea Hospitali ya Kairuki iliyopo Mikocheni Jijini Dar na kujionea huduma za kisasa zinavyotolewa hospitalini hapo.
Mabalozi hao wakiwa hospitalini hapo walitembelea vitengo mbalimbali kama vile kitengo cha wagonjwa wa dharura, upasuaji, wadi ya wazazi na wadi maalum na kujionea mitambo ya kisasa inayotumika kuangalia afya za wagonjwa.

Pamoja na mitambo hiyo walijionea mtambo mpya kabisa wa MRI unaotumika kubaini tatizo la mgonjwa kama ilivyokuwa kwa mashine ya CT Scan ambayo imepitwa na wakati kwa mtambo huo.

Akizungumza baada ya kuwapokea mabalozi hao, Mkurugenzi wa Hospitali hiyo, Dkt. Asser Mchomvu amesema mtambo huo wa MRI ni wakisasa kabisa ambapo kabla yake ulikuwa ukitumika mtambo wa CT Scan lakini kutokana na hospitali yao kwenda na wakati kila kukicha wameamua kuleta mtambo huo ambao hutumika kwa nchi zilizoendelea.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Mtandao wa Elimu na Afya (Kairuki Health and Education Network- KHEN) ambayo inaunganisha Kairuki Hospital na Hubert Kairuki Memorial University and School of Nursing, Kokushubira Kairuki aliwakaribisha mabalozi hao kwenye hospitali hiyo na kuwaambia endapo wananchi katika nchini wanazotoka watakumbwa na changamoto za kiafya wasisite kufikia hospitalini hapo kwa ajili ya kupata huduma za uhakika.

Balozi wa Comoro hapa nchini, Dkt. Ahmada El Badasui alipongeza huduma zinazotolewa kwenye hospiatali hiyo na kusema ni za kiwango cha juu na kuzifanisha na nchi zilizoendelea.

“Kiukweli huduma zinazotolewa hapa ni za kiwango cha juu sana hivyo naupongeza uongozi wa hospitali kuweza kwenda na wakati kufikia kiasi cha kuwa na mtambo huo wa kisasa wa MRI”. Alisema Balozi wa Comoro.

Balozi Mdogo wa Burundi, Prefere Ndayishimiye amesema kwa upande wake anaupongeza sana uongozi wa hospitali kwa kufikia mafanikio hayo ambayo ni maendeleo ya bara la Afrika kwa ujumla.

“Maendeleo haya ni ya Afrika kwa ujumla ukweli huduma tulizozishuhudia ni za kisasa kabisa haswa ule mtambo wa MRI ambao ni nchi chache za afrika waliokuwa nao”. Alisema Balozi huyo.

HABARI/PICHA ZOTE NA RICHARD BUKOS /GPL