The House of Favourite Newspapers

Kambi ya Yanga Kama Ulaya, Avic Kigamboni Dar

0

NI sahihi kusema kuwa kambi ya Yanga ni kama Ulaya, baada ya waandishi wetu kwenda kuitembelea jana na kushuhudia mambo makubwa.

Kuanzia msimu huu umeanza Yanga wamekuwa wakikaa kwenye kambi ya kisasa eneo la Avic Kigamboni na mara kwa mara imekuwa adimu sana kwa waandishi kufika hapo.

 

Jana Championi ilitembelea kambi hiyo na kushuhudia wachezaji wa timu hiyo wakiishi kama vile wapo Ulaya, sehemu ya kisasa yenye utulivu wa hali ya juu.

 

Eneo la kambi hiyo ambalo lipo kwenye mandhari nzuri, lina nyumba ndogondogo zaidi ya 50, mabwawa ya kuogelea mawili, gym moja yenye vifaa vyote vya kisasa na viwanja viwili, kimoja na mchezo wa kikapu na kingine cha soka.

Kuonyesha kuwa sasa Yanga wanaishi kwenye kambi bora, eneo hilo ndiyo wanakaa wachezaji wote, makocha pamoja na madaktari wa timu hiyo na ni eneo lenye ulinzi mkali saa 24.

 

“Ni ngumu sana mtu kuingia hapa, kuna ulinzi saa 24 na kama hufahaminiki huwezi kuingia, hata ndugu wa mchezaji akitaka kuja huku lazima kuwe na taarifa maalum ya maandishi hapo getini ndiyo aweze kuingia.“

Huwezi kuihujumu timu ikiwa hapa kwa kuwa hakuna anayeweza kupiga picha wala kutazama mazoezi ya timu, hakika huku kila kitu kinakwenda kisasa sana,” alisema mfanyakazi mmoja ndani ya majengo hayo.

Kuna eneo la jiko, mikutano na sehemu ya wachezaji kucheza michezo mingine ikiwemo table tenisi na mingine mingi.Waandishi ambao walipelekwa kushuhudia kila kitu kinavyokwenda hapo, walielezwa maandalizi ya kila timu ile ya vijana, wakubwa na hata ya wanawake ambapo kila kitu kilionekana kwenda kwa utaratibu mzuri.

Mkurugenzi wa Uwekezaji wa GSM, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili Yanga, Hersi Said akizungumza jana alisema kutokana na kambi hiyo na mambo mengine ambayo Yanga wamefanya ni dhahiri kuwa sasa timu hiyo kufungwa ni ngumu.

“Kwanza kwenye suala la ushindi kwa sasa nafikiri ni jambo la muhimu kwenye kila mchezo na ukitazama tumewaleta wachezaji mahiri akiwemo Fiston ambaye ni mtambo wa mabao, nafikiri sasa suala la kushinda bao moja moja kwetu ilikuwa mwisho mzunguko wa kwanza, Wanayanga wasiwe na wasiwasi kwani sasa tuna safu imara sana ya ushambuliaji,” alisema kigogo huyo.

 

Yanga ndiyo wanaongoza Ligi Kuu Bara wakiwa na pointi 44 baada ya kucheza michezo 18 wameshinda kumi na tatu na kutoka sare mitano wakiwa hawapoteza mchezo hata mmoja kadi sasa.

⚫️ Kwa UPDATES zote, Download GLOBAL APP: ⚫️ ANDROID:http://bit.ly/38Lluc8 ⚫️ iOS:https://apple.co/38HjiCx

Leave A Reply