The House of Favourite Newspapers

Gomes Afunguka Ishu ya Mshambuliaji Mpya Simba

0

MABAO ambayo wameyafunga washambuliaji watatu wa klabu ya Simba, John Bocco, Chris Mugalu na Meddie Kagere yamempa kigugumizi kocha mkuu wa timu hiyo, Didier Gomes kuhusiana na usajili wa mshambuliaji mpya ndani ya kikosi hicho.

 

Kabla ya mchezo wa jana kwenye kikosi cha Simba washambuliaji hao walikuwa tayari wamefunga jumla ya mabao 40, ambapo kinara alikuwa ni nahodha wao Bocco ambaye alikuwa na mabao 15, akifuatiwa na Mkongomani Chris Mugalu mwenye mabao 13, huku mfungaji bora wa misimu miwili mfululizo iliyopita Meddie Kagere yeye akiwa ameweka kambani mabao 12.

 

Simba imekuwa ikihusishwa na usajili wa baadhi ya majina makubwa ya washambiuliaji wakiwemo Walter Bwalya wa Al Ahly, Kadima Kabangu wa DC Motema Pembe na Emmanuel Okwi.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, kuhusu usajili wa straika mpya ndani ya kikosi hicho Gomes alisema: “Kwanza ningependa kuweka wazi kuwa nina furaha kubwa na ubora wa washambiuliaji wote watatu walio ndani ya kikosi changu.

 

“Kuhusu ikiwa tunahitaji kusajili mshambuliaji mpya msimu ujao, inawezekana likawa ni wazo zuri lakini siwezi kusema tuna ulazima sana wa kufanya hivyo.”

JOEL THOMAS, Dar es Salaam

Leave A Reply