
WAKATI yakisubiriwa kwa hamu maamuzi ya Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Michezo (CAS), kuhusiana na kesi ya Yanga dhidi ya kiungo mshambuliaji wa Simba, Bernard Morrison kila upande umeonekana kuwa na matumaini makubwa ya kushinda huku tambo zikiendelea kutembea.
Kesi hiyo yenye usajili wa CAS 2020/A/7397 ilisikilizwa juzi Alhamisi Juni 29, mwaka huu ambapo baada ya kusikiliza mashauri ya pande zote mbili, mahakama hiyo iliweka wazi kuwa majibu ya kesi hiyo yatatolewa Agosti Mosi mpaka 24, mwaka huu.
Katika kesi hiyo uongozi wa Yanga unadai uliingia na makubaliano ya mkataba wa miaka miwili na mchezaji huyo, huku Morrison yeye akidai kuwa mkataba wake halali ulikuwa wa miezi sita pekee ambao uliisha Julai 2020.
Akizungumza na Championi Jumamosi, Msemaji wa Yanga, Hassan Bumbuli alisema: “Tunamshukuru Mungu kesi imeenda vizuri na baada ya taratibu zote za mashauri ya kesi kufanyika, sasa hivi utaratibu wa kawaida wa kufanya tathmini ya ushahidi uliotolewa hivyo watatoa maamuzi kati ya Agosti mosi mpaka 24 mwaka huu.
“Ni kweli hatuwezi kuzungumzia hatima ya kesi hii, lakini tuna matumaini makubwa haki
itatendeka hivyo Wanayanga wanapaswa kuwa watulivu wakati huu mahakama ikiwa inafanya maamuzi yake.”Kupitia mtandao wa Instagram, Morrison aliandika: “Hata katika wingi wa maji, bado mjinga ataendelea kuhisi kiu.”
Stori: JOEL THOMAS,Dar es Salaam