
Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi imetupilia mbali pingamizi lililowekwa na mawakili wa utetezi kumkataa shahidi wa Jamhuri, Askari Polisi, Ricardo Msemwa aliyekuwa na simu, kalamu na diary wakati akitoa ushahidi katika kesi ya Ugaidi inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake watatu.
Jaji Joachim Tiganga ametupiliambali pingamizi hilo leo Jumatano Novemba 17, 2021 katika uamuzi mdogo wa pingamizi lililowekwa Ijumaa na upande wa utetezi nakuagiza mawakili wa pande zote kukagua diary hiyo.
Sehemu ya uamuzi wa Jaji Tiganga;
Jaji: Lakini kwa jambo hilo Mahakama ina maamuzi kwamba nyaraka yoyote inayojitokeza kwenye mwenendo wa kesi mahakamani basi itakuwa ni nyaraka ama kielelezo cha Mahakama. Na kwamba kwa sababu notebook hiyo ilikutwa kwenye kizimba cha mahakama hii basi upande wa utetezi … Lakini Mahakama ina maoni kwamba kuhusu taarifa za siri zilizokuwa katika notebook hiyo zinaweza kuangukia katika mikono ya watu wasiohusika.
Jaji: Kwa Namna hiyo basi, kwa sababu jambo hilo linahusu haki za watu, Mahakama inaweka utaratibu wa wakili mmoja mmoja ataruhisiwa kukagua na kwa sehemu husika tu. Na wakili hataruhusiwa kupiga picha sehemu ya notebook hiyo.
Jaji: Hiyo ndiyo maana ya kauli yangu kwamba ‘haki isitendeke tu, bali ionekane ikitendeka.’ Na huo ndio uamuzi wangu.
(Mawakili wa pande zote mbili wanasimama kukubaliana na Jaji).
Jaji: Mniambie maoni yenu mkafanyie zoezi hili katika usiri au hata hapahapa. Nahitaji maoni yenu
(Mawakili wa pande zote mbili wanashauriana).
Wakili wa Serikali: (Robert Kidando) Kama ukiridhia naomba uahirishe shauri kwa muda kwa sababu hatuwezi kujua ukaguzi utachukua muda gani.
Jaji: Utetezi ni sawa?
Kibatala: Sawa. Haina Shida. kwa dakika 20 inatosha.
Jaji: Kwa sababu nimesema taarifa yoyote isichukuliwe kwa picha au vinginevyo, basi namweka na afisa wangu mmoja kwa ajili ya kusimamia hilo zoezi.
(Mawakili wa pande zote mbili wanakubaliana kuhusu hilo).