Marehemu Mafwiri Mfungo, enzi za uhai wake.
Stori: Gabriel Ng’osha, Dar na Gregory Nyankaira, Mara
VILIO na majonzi vilitawala nyumbani kwa mzee Mfungo Mtaengelwa wakati wa mazishi ya kijana wake, Mafwiri Mfungo, 28, aliyekuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), aliyeuawa kwa kupigwa risasi tatu kifuani na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi. Tukio hilo linalowaliza wanachuo wenzake mpaka sasa, lilijiri Desemba 15, mwaka huu, Ubungo Msewe jijini Dar es Salaam.
Jeneza lenye mwili wa marehemu.
ALIYEKUWA NAYE ASIMULIA
Beatus Chrispian ambaye alikuwa rafiki mkubwa wa Mafwiri, wakiishi nyumba moja na aliyekuwa na marehemu hadi dakika za mwisho, anasema yeye alinusurika katika tukio hilo baada ya kujeruhiwa kwa risasi tumboni.
Beatus Chrispian aliyejeruhiwa.
Alisema: “Siku ya tukio tulikuwa ndani, saa 2 usiku, tukipanga mipango ya kesho yake. Ghafla tulisikia mlipuko mkubwa nje.
“Tulitoka nje na kuona cheche za moto zikitokea karibu na transfoma moja ya umeme. Tukadhani huenda transfoma hiyo ilikuwa inalipuka, tukaenda ili kushuhudia kama ni kweli tuwajulishe Tanesco.”
Beatus akiwa na jeraha tumboni.
MAREHEMU ANASHIKILIA TUMBO
“Kabla hatujafika, ghafla nikamwona marehemu anainama na kushikilia tumbo huku akilia kwa uchungu. Na mimi nikasikia kama kitu cha baridi kimenichoma tumboni. Ilibidi nikimbilie ndani. Nikashangaa kuona damu zinanitoka tumboni, nikagundua kumbe nilikuwa nimepigwa risasi. Muda mfupi baadaye nikasikia vilio vya watu huku wakilitaja jina la Mafwiri… Mafwiri. “Nilipojikaza na kwenda eneo hilo, nilimkuta Mafwiri amelala chini, kumbe alishafariki dunia. Alikuwa na majeraha matatu ya risasi kifuani.”
Kabuli la marehemu Mafwiri
KILICHOJULIKANA
Beatus alisema, baada ya tukio hilo ilibainika kuwa maduka matano, likiwemo moja la pesa yalikuwa yameporwa fedha na majambazi hao. “Inaonekana sisi tulipokwenda, walituona, wakajua tunawafuatilia
ndiyo maana wakatupiga risasi,” alisema Beatus akiwa na jeraha tumboni.
HISTORIA FUPI YA MAREHEMU
Marehemu Mafwiri wakati wa uhai wake, baada ya kuhitimu kidato cha sita na kozi ya ufundi katika Chuo cha Ufundi Moshi, Kilimanjaro, aliajiriwa na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) jijini Mwanza, 2009. Mwaka 2012, alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam akisomea shahada ya uhandisi (Engineering) hadi alipofikwa na mauti. Pia alikuwa Naibu Waziri wa Miundombinu katika serikali ya wanafunzi chuoni hapo.
MAZISHI YAKE
Marehemu Mafwiri alizikwa Desemba 20, mwaka huu nyumbani kwao, Kitongoji cha Sabasaba, Kijiji cha Nyamisisi, Wilaya ya Butiama mkoani Mara. Ameacha watoto wawili.

….waombolezaji.