×

Emirates Kuanza Kutangaza Vivutio Vya Utalii Vya Tanzania

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt.Damas Ndumbaro amefanya mazungumzo na Uongozi wa juu wa Shirika la ndege la Umoja wa Falme za Kiarabu la Emirates kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo Tanzania ambapo  vitaweza kuonwa na  abiria wapatao  milioni  90.2 wanaosafiri kila  mwaka kupitia ndege za shirika hilo.

Aidha, tangazo la vivutio vya utalii vya Tanzania litakuwa likitazamwa na mamilioni ya abiria wa Shirika hilo wakati ndege zitakapokuwa zikiruka (take off) katika viwanja mbalimbali duniani.

Waziri Ndumbaro amebainisha hayo Dubai  alipokutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Shirika hilo ambalo mbali na kusafirisha abiria milioni 90.2 duniani kote  pia  husafirisha abiria wapatao milioni 20 ambao huunganisha ndege nyingine.

Katika hatua nyingine, Dkt.Ndumbaro amesema katika mazungumzo hayo wamekubaliana  ziandaliwe makala tano (Documentaries ) za kuelezea vivutio vya utalii vya Tanzania ikiwemo  Zanzibar, Serengeti, Ngorongoro pamoja  na Mlima Kilimanjaro.

” Shirila la ndege la Emirates ni  Shirika kubwa sana Duniani lengo letu kama nchi  ni kuhakikisha abiria wapatao milioni 90.2 wanaviangalia vivutio vyetu kisha wanavipenda halafu wanatembelea Tanzania” amesisitiza Dkt. Ndumbaro.

Ameongeza kuwa katika mazungumzo hayo uongozi wa ndege hizo  umeonesha utayari wa kushirikiana na Tanzania kutangaza utalii na ifikapo mwanzoni mwa mwezi wa Mei mwaka huu wataingia makubaliano (MOU) baina ya Tanzania na Shirika hilo

Dkt.Ndumbaro amesema kati ya abiria watakaoangalia vivutio hivyo watavutiwa na hatimaye sehemu ya watu hao waweze  kuja kutembelea  Tanzania

” Shabaha yetu kubwa kama nchi ni kuhakikisha tunafikia watalii milioni 5 ifikapo mwaka 2025, Tunaamini tutalifikia lengo hilo” amesisitiza Dkt.Ndumbaro

Amesema Tanzania inategemea utalii wake wa Wanyamapori  kwa asilimia 100 hivyo kupitia mkakati wa kutangaza vivutio vingine vya utalii kama vile utalii wa fukwe, utalii wa utamaduni pamoja na utalii wa ikolojia itawezesha utalii huo kujulikana dunia kote na kuwa chachu ya watalii kumiminika nchini Tanzania.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Masoko wa Afrika wa Shirika la ndege la Umoja wa Falme za Kiarabu  la Emirates, Badr Abbas amesema Shirika la Emirate lipo tayari kufanya kazi na Tanzania katika kuhakikisha vivutio vya utalii vya Tanzania vinajulikana.

” Tutakapofikia makubaliano tutahakikisha pia matangazo ya vivutio vya Utalii wa Tanzania yanawekwa kwenye Tovuti pamoja na mitandao ya kijamii ikiwemo facebook, instagram pamoja na twitter ya Shirika hili ambayo imekuwa ikifuatiliwa na watu wengi Duniani.

Kwa upande wake, Balozi Mdogo wa Dubai, Mhe. Idd Bakari amesema mazungumzo yamekuwa na tija na hivyo kupitia Shirika hilo idadi ya watalii itaongezeka kupitia matangazo yatakayokuwa yakiruka wakati ndege za Shirika hilo zitapokuwa zikiruka

” Mazungumzo haya baina yetu na Shirika la Emirates yataipaisha Tanzania vivutio vya utalii vitaweza kujulikana Duniani kote kuwa vipo Tanzania na hivyo watalii wengi watweza kuitembelea Tanzania

Katika mazungumzo hayo Ujumbe wa Tanzania umeongozwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro pamoja na Balozi Mdogo wa Tanzania, Mhe.Idd Bakari.

Leave a Comment