
UONGOZI wa Yanga, umethibitisha kuwa, kiungo wa timu hiyo, Khalid Aucho, yupo fiti kwa asilimia 100, ambapo ameruhusiwa kujiunga na Timu ya Taifa ya Uganda, huku Yanga wakitumia hiyo kama sehemu ya kumuandaa kuivaa Azam FC.
Aucho ni miongoni mwa mastaa ambao wamejumuishwa katika kikosi cha timu ya Taifa ya Uganda kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wao wa kimataifa wa kirafiki dhidi ya Tajikistan, unaotarajiwa kupigwa kesho Ijumaa.
Kiungo huyo raia wa Uganda, alikosekana katika michezo miwili ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Geita Gold na KMC, kutokana na majeraha ya misuli, lakini sasa yupo fiti kucheza dhidi ya Azam, Aprili 6, mwaka huu.
Akizungumzia hali ya Aucho, Mtaalamu wa Viungo na Daktari wa Yanga, Youssef Mohammed, alisema: “Kuhusu hali ya Aucho mashabiki wa Yanga hawapaswi kuwa na wasiwasi kwani tayari ameshapona kwa asilimia 100 ndiyo maana aliruhusiwa kujiunga na kikosi cha Timu ya Taifa ya Uganda.
“Tunaamini kama atapata nafasi ya kutumika katika mchezo huo wa kimataifa basi itakuwa kipimo kizuri zaidi kwake kuwa sawa, kabla hajarejea na kuungana na timu kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wetu dhidi ya Azam.”