×

Visu Vipya Vya Yanga Hadharani Mapinduzi Cup, Luis Miquissone na Bobosi Watajwa

UONGOZI wa Yanga umeweka wazi kuwa utatambulisha majembe mawili mapya kabla ya mchezo wao wa kwanza wa michuano ya Kombe la Mapinduzi kuanza.

Yanga kwa sasa wamekuwa wakihusishwa kwa karibu na usajili wa wachezaji wawili wakiwemo Luis Miquissone na Bobosi Byaruhanga kupitia dirisha hili dogo la usajili.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Ofisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe alisema kuwa Yanga kabla ya kucheza mchezo wao wa kwanza wa Mapinduzi basi watatambulisha majembe hayo mawili mapya ambayo tayari wameshakamilisha usajili jambo ambalo amewaahidi Wananchi wakae mkao wa kula.

Bobosi Byaruhanga

“Kabla ya Mapinduzi Cup tutakuwa tayari tumeshafanya usajili wa wachezaji wetu wapya, tutatambulisha vyuma vyetu viwili vya maana ambavyo vitaenda kutetemesha nchi kwa kuwa ni wachezaji wa maana na wenye uwezo mkubwa.

“Wananchi wanatakiwa wafahamu kwanza kabla ya michuano ya Mapinduzi kuna furaha kubwa ya kutambulisha majembe yetu ambayo tunaamini kuwa watayapokea na watayafurahia zaidi kutokana na uwezo wao kuwa mkubwa na wa kipekee, lazima usajili huo uweze kutetemesha nchi,” alisema Kamwe.

Stori na Marco Mzumbe

Leave a Comment