
Rais wa Marekani Donald Trump ameongeza vitisho dhidi ya Iran akisema taifa hilo linaweza “kuondolewa ndani ya usiku mmoja,” huku vita kati ya pande hizo ikiingia wiki ya sita.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari White House usiku wa kuamkia leo Aprili 7, 2026 Trump alidai kuwa Marekani ina mpango wa kushambulia miundombinu muhimu ya Iran, ikiwemo madaraja na vituo vya umeme, ikiwa mzozo utaendelea.
Kauli hiyo imekuja wakati Iran ikikataa mapendekezo ya kusitisha vita kwa muda, ikisema hatua hiyo ingeipa nafasi Marekani na washirika wake kujipanga upya kwa mashambulizi zaidi.
Pamoja na vitisho hivyo, Trump alisema mazungumzo ya kumaliza vita yanaendelea vizuri kupitia wapatanishi, lakini akasisitiza kuwa hali bado ni nyeti sana.
Kwa upande wake, Israel imeidhinisha orodha mpya ya malengo ya kushambulia, hasa katika sekta ya nishati, iwapo juhudi za kidiplomasia zitashindikana.
Iran Yajibu kwa Vitisho na Masharti
Maafisa wa Iran nao hawakubaki kimya, wakisema mlango wa Strait of Hormuz hautafunguliwa tena hadi fidia ya uharibifu wa vita ilipwe na mashambulizi kusitishwa kabisa.
Iran imewasilisha masharti kadhaa, ikiwemo:
- Kusitishwa kwa vita katika ukanda mzima
- Usalama wa usafirishaji kwenye Strait of Hormuz
- Kuondolewa kwa vikwazo vya kiuchumi
Mapigano Yaendelea kuwa mbaya zaidi:
- Mashambulizi ya Israel yamelenga miundombinu ya petrochemical ya Iran, ikiwemo South Pars, hatua inayotajwa kuwa pigo kubwa kiuchumi.
- Katika Tehran, watu kadhaa wameripotiwa kufariki baada ya mashambulizi kulenga maeneo ya makazi.
- Nchini Lebanon, watu zaidi ya 1,400 wameuawa tangu vita ianze, huku maelfu wakikimbia makazi yao.
- Katika mji wa Haifa, watu wanne waliuawa baada ya shambulio la kombora.