×

Trump Atoa Onyo Iran na Israel Kusitisha Mashambulizi, Houthis Waingia Kwenye Vita – Video

Rais wa Marekani Donald Trump ameitaka Iran na Israel kusitisha mara moja mashambulizi yao ya kulipizana kisasi huku hali ya usalama Mashariki ya Kati ikiendelea kuwa tete na kuhatarisha mazungumzo ya kusaka suluhu ya vita hivyo.

Trump aliandika kupitia mtandao wake wa Truth Social akisema, “Israel na Iran lazima waache mara moja kushambuliana.”

Kwa upande wake, Iran imeishutumu Marekani kwa kuhusika moja kwa moja na kuendelea kwa mashambulizi hayo, ikidai kuwa hatua za Israel haziwezi kutenganishwa na sera za Marekani. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmaeil Baqaei, amesema hakuna anayeamini kuwa Israel inaweza kufanya mashambulizi bila uratibu na ushirikiano wa Marekani.

Wakati mvutano huo ukiendelea, Israel imesema imefanya mashambulizi katika kiwanda cha petrokemikali cha Mahshahr kusini-magharibi mwa Iran pamoja na maeneo mengine ya kijeshi. Iran nayo kupitia Walinzi wa Mapinduzi ilidai kujibu kwa kurusha makombora kuelekea kiwanda kama hicho katika mji wa Haifa nchini Israel.

Milipuko mikubwa pia ilisikika katikati ya mji wa Tehran huku mifumo ya ulinzi wa anga ikianza kufanya kazi. Vyombo vya habari vya Iran viliripoti kuwa droni iliyodaiwa kuwa ya “adui wa Marekani na Israel” ilidunguliwa juu ya anga la Tehran.

Trump amesema mashambulizi hayo hayatavuruga juhudi za kufikia makubaliano ya amani kati ya Marekani na Iran, akisisitiza kuwa yeye ndiye mwenye maamuzi makubwa katika mchakato huo na si Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu.

Katika hatua nyingine, kundi la Houthis kutoka Yemen limetangaza kuongeza mashambulizi dhidi ya Israel na kupiga marufuku meli zinazohusishwa na Israel kupita katika Bahari ya Shamu, likisema hatua hiyo ni sehemu ya mshikamano wao na “mhimili wa upinzani” unaojumuisha Iran, Lebanon, Iraq na Gaza.

Mvutano huo umeendelea kuongeza hofu ya kuongezeka kwa vita vikubwa Mashariki ya Kati huku mazungumzo ya kusitisha mapigano yakiwa hatarini kuvunjika kabisa.

Leave a Comment