
Viongozi wa Marekani na Pakistan wametangaza matarajio ya kusainiwa kwa makubaliano ya awali ya amani kati ya Marekani na Iran siku ya leo Jumapili Juni 14, 2026 hatua inayolenga kumaliza vita vilivyodumu kwa zaidi ya miezi mitatu kati ya mataifa hayo mawili.
Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali, wapatanishi kutoka Qatar waliwasili Tehran mapema Jumapili kwa ajili ya kukamilisha mazungumzo ya mwisho kuhusu makubaliano hayo. Rais wa Marekani Donald Trump amesema makubaliano hayo yalitarajiwa kusainiwa siku ya kuzaliwa kwake, huku Waziri Mkuu wa Pakistan Shehbaz Sharif akieleza kuwa pande zote zimekubaliana kuhusu mfumo wa awali wa mkataba wa amani.
Hata hivyo, Iran imeendelea kuwa na tahadhari kuhusu muda rasmi wa kusainiwa kwa makubaliano hayo. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmaeil Baghaei, amesema kuwa makubaliano hayo huenda yasitiwe saini mara moja bali katika siku zijazo baada ya mazungumzo zaidi kukamilika.
Moja ya masuala makubwa yanayobaki mezani ni hatima ya Mlango wa Hormuz, njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta duniani. Iran imekuwa ikiudhibiti mlango huo tangu kuanza kwa vita, jambo lililosababisha misukosuko katika masoko ya kimataifa. Trump amesema kuwa baada ya kusainiwa kwa makubaliano hayo, Mlango wa Hormuz utafunguliwa mara moja kwa matumizi ya kimataifa.
Pia suala la mpango wa nyuklia wa Iran linaendelea kuwa kikwazo kikubwa katika mazungumzo hayo. Marekani imekuwa ikisisitiza kuondolewa au kuharibiwa kwa akiba ya uranium iliyorutubishwa, huku Iran ikisisitiza kuwa malighafi hiyo ishughulikiwe ndani ya mipaka yake.
Wakati juhudi za kidiplomasia zikiendelea, bado kumeshuhudiwa matukio ya kijeshi katika eneo la Hormuz. Jeshi la Marekani limedai kudungua ndege kadhaa zisizo na rubani zilizorushwa na Iran kuelekea meli za kibiashara zilizokuwa zikivuka eneo hilo.