×

Ufaransa Kukutana na Mtihani wa Morocco Robo Fainali Kombe la Dunia

NEW YORK: Kampeni ya Ufaransa katika Kombe la Dunia imekuwa ikijaribu uwezo wao wa kushambulia, uvumilivu na utulivu wa akili, lakini mchezo wa robo fainali dhidi ya Morocco siku ya Alhamisi unatarajiwa kuwa mtihani wao mkubwa zaidi wa soka katika mashindano haya.

Mchezo huo utakuwa marudiano ya nusu fainali ya Kombe la Dunia 2022 nchini Qatar, ambapo Ufaransa iliivunja ndoto ya Morocco kufika fainali. Hata hivyo, safari hii Morocco haiji kama timu ya kushtukiza, bali kama kikosi chenye kujiamini, uwezo mkubwa na wazi kimeweka lengo la kutwaa ubingwa.

Ufaransa ilitinga hatua ya robo fainali baada ya kuifunga Paraguay kwa bao 1-0 katika mchezo uliowahitaji zaidi uvumilivu na uwezo wa kuvunja ukuta wa ulinzi kuliko kucheza soka la kuvutia.

Kocha Didier Deschamps na kikosi chake walifanikiwa kupata ushindi huo kupitia bao la Kylian Mbappe, ambaye limekuwa bao lake la saba katika Kombe hili la Dunia. Hata hivyo, mchezo huo uliibua maswali kuhusu uwezo wa Ufaransa kuvuka vizuizi vigumu katika hatua za mtoano.

Dhidi ya Morocco, changamoto itakuwa tofauti kabisa. Kikosi cha kocha Mohamed Ouahbi kimeonyesha uwezo wa kuvumilia presha, kumiliki mpira kwa vipindi na kuwaadhibu wapinzani kwa kasi na umakini mkubwa.

Ushindi wa Morocco wa mabao 3-0 dhidi ya Canada katika hatua ya 16 bora umeonyesha kuwa timu hiyo inaendelea kuimarika kadri mashindano yanavyoendelea baada ya kumaliza hatua ya makundi bila kupoteza mchezo.

Morocco tayari ilionyesha ubora wake katika kundi lenye ushindani mkubwa, ikikusanya pointi saba dhidi ya Brazil, Scotland na Haiti. Matokeo hayo yameongeza imani yao kwamba hawapo nchini humo kwa ajili ya kurudia tu mafanikio ya kihistoria ya mwaka 2022, bali kupigania taji.

Kwa upande mwingine, Ufaransa bado haijakutana na timu yenye mchanganyiko wa ubora wa kiufundi, nguvu za kimwili na kujiamini kama Morocco. Sweden iliondolewa kwa urahisi katika hatua ya 32 bora, huku Paraguay ikitoa upinzani lakini bila kuwa na tishio kubwa la kisoka kama Morocco inavyotarajiwa.

Robo fainali hiyo itakuwa kipimo kikubwa kuona kama safu ya ushambuliaji ya Ufaransa itaendelea kutawala dhidi ya timu yenye uwezo wa kuwashambulia kwa mipira ya kushtukiza na kujaribu kuvuruga uwiano wao wa ulinzi.

Ufaransa huenda ikakosa huduma ya kiungo Aurélien Tchouaméni kutokana na majeraha ya misuli, wakati Morocco nayo inatarajiwa kuwa bila mshambuliaji muhimu Ismael Saibari.

Mbali na Mbappe, Ufaransa inategemea uwezo wa Ousmane Dembélé, Michael Olise na Bradley Barcola, ambao wameifanya safu yao ya mbele kuwa moja ya hatari zaidi katika mashindano haya.

Hata hivyo, nidhamu ya Morocco, mpangilio wao wa mchezo na kujiamini kwao vinatarajiwa kutoa kipimo kamili kwa ubora halisi wa Ufaransa katika hatua hii muhimu ya Kombe la Dunia.

Leave a Comment