×

Mwanamitandao wa Ghana Apelekwa Marekani Kujibu Tuhuma za Ulaghai wa Kimapenzi

Mtengeneza maudhui maarufu wa mitandao ya kijamii kutoka Ghana, Frederick Kumi, anayejulikana zaidi kwa jina la Abu Trica, amesafirishwa kwenda Marekani kujibu mashtaka yanayomhusisha na mtandao wa ulaghai wa kimapenzi mtandaoni uliodaiwa kuwaibia wazee wa Marekani zaidi ya dola milioni nane.

Kumi, mwenye umri wa miaka 28 na mkazi wa Swedru kusini mwa Ghana, alipelekwa Marekani Alhamisi kwa ndege ya Delta Airlines, licha ya mawakili wake kudai kuwa walikuwa wamewasilisha ombi mahakamani la kusitisha hatua hiyo hadi uhalali wa kurejeshwa kwake nchini humo uamuliwe.

Wakili wake, Oliver Barker Vormawor, alisema serikali ilichukua hatua ya kumsafirisha mteja wake kabla mahakama haijatoa uamuzi kuhusu ombi hilo, jambo ambalo amesema linaibua maswali kuhusu kuheshimiwa kwa mchakato wa mahakama.

Mamlaka za Marekani zilimfungulia Kumi mashtaka mwezi Desemba mwaka jana yakiwemo kula njama za kufanya ulaghai wa kielektroniki, kula njama za kutakatisha fedha na makosa mengine yanayohusiana na uhalifu wa kifedha. Endapo atapatikana na hatia, anakabiliwa na kifungo cha hadi miaka 20 jela.

Kukamatwa kwake kulitokana na operesheni ya pamoja iliyofanywa na vyombo vya usalama vya Ghana na Marekani, iliyolenga kuvunja mitandao ya ulaghai wa mtandaoni inayowaathiri wazee.

Kwa mujibu wa waendesha mashtaka wa Marekani, Kumi na mshukiwa mwenzake, Emmanuel Kojo Baah Obeng, walidaiwa kutumia teknolojia ya akili bandia (AI) kuunda utambulisho wa watu wasio halisi kwenye mtandao ili kuwavutia waathiriwa katika mahusiano ya kimapenzi.

Inadaiwa kuwa baada ya kujenga uaminifu kupitia simu, barua pepe na programu za kutumiana ujumbe, waliwaomba waathiriwa kutuma fedha wakidai zinahitajika kwa dharura za matibabu, gharama za usafiri au fursa za uwekezaji ambazo hazikuwa za kweli.

Waendesha mashtaka wanadai fedha zilizotumwa zilisambazwa kwa washirika waliokuwa nchini Marekani na Ghana kupitia akaunti mbalimbali ili kuficha chanzo chake.

Kesi hiyo ni sehemu ya juhudi za mamlaka za Marekani za kukabiliana na ongezeko la ulaghai unaowalenga wazee kupitia mtandao, hasa ulaghai wa kimapenzi ambao umeendelea kusababisha hasara kubwa za kifedha kwa waathiriwa.

Leave a Comment