
LONDON: Prince Harry na mkewe, Meghan Markle, wameamua kurejea kuishi nchini Uingereza, lakini hawatarejea katika majukumu yao kama wajumbe wanaofanya kazi rasmi wa familia ya kifalme, vyombo vya habari vya Uingereza vimeripoti.
Kwa mujibu wa Daily Telegraph, watoto wao wawili, Prince Archie, mwenye miaka saba, na Princess Lilibet, mwenye miaka mitano, tayari wameandikishwa katika shule nchini Uingereza na wanatarajiwa kuanza masomo mwezi Septemba.

Familia hiyo inatarajiwa kuishi katika makazi binafsi yasiyo ya kifalme nje ya London.
Harry na Meghan waliacha majukumu yao rasmi ya kifalme na kuhamia California zaidi ya miaka sita iliyopita, ambako walianza kujitegemea kifedha kupitia mikataba mbalimbali ya kibiashara, ikiwemo mikataba na Netflix na Spotify.
Tangu walipoondoka Uingereza, uhusiano wao na baadhi ya wanafamilia wa kifalme umekuwa na misukosuko. Hata hivyo, katika kipindi cha hivi karibuni, Harry ameonyesha nia ya kupatanisha uhusiano wake na familia yake, hasa na baba yake, King Charles III, ambaye anaendelea kupata matibabu ya saratani.
Ripoti zinasema Charles alifahamishwa kuhusu mpango huo siku ya Jumapili, huku akiwa hakuelezwa kuhusu uamuzi huo wakati Harry na Meghan walipomtembelea nchini Uingereza mwezi uliopita.
Buckingham Palace ina sera ya kutotoa maoni kuhusu taarifa za uvumi zinazowahusu wanafamilia wa kifalme ambao si wajumbe wanaofanya kazi rasmi. Msemaji wa Harry na Meghan pia amekataa kutoa maoni kuhusu taarifa hizo.
Uhusiano wenye misukosuko na familia ya kifalme
Harry na Meghan wamekuwa na uhusiano wenye misukosuko na familia ya kifalme tangu walipoondoka Uingereza na kuhamia katika eneo la Montecito, California.
Katika mahojiano mbalimbali pamoja na kitabu chake cha kumbukumbu Spare, Harry alieleza sababu zilizowafanya kuondoka Uingereza, akidai kuwa walikabiliwa na vikwazo na shinikizo kubwa kutokana na maisha ya kifalme.
Wawili hao pia waliikosoa familia ya kifalme na maofisa wa ikulu kuhusu namna walivyoshughulikia changamoto za Meghan za afya ya akili. Aidha, walidai kuwa mmoja wa wanafamilia wa kifalme aliwahi kutoa kauli kuhusu rangi ya mtoto wao wakati Meghan alipokuwa mjamzito wa mtoto wao wa kwanza.
Meghan amekuwa akijieleza kuwa ana asili ya mchanganyiko wa rangi.
Mzozo wa Harry na vyombo vya habari
Mvutano huo uliendelea kuongezeka kutokana na vita vya muda mrefu vya Harry dhidi ya baadhi ya magazeti ya udaku nchini Uingereza.
Harry amekuwa akidai kuwa simu zake zilidukuliwa kinyume cha sheria na kwamba faragha yake ilivamiwa alipokuwa mdogo. Hata hivyo, amepoteza kesi kadhaa alizofungua dhidi ya vyombo vya habari, ikiwa ni pamoja na kesi dhidi ya kampuni inayochapisha Daily Mail.
Kesi hiyo ya hivi karibuni imemuweka Harry katika hatari ya kulipa mamilioni ya pauni kutokana na gharama za kisheria. Associated Newspapers imewasilisha nyaraka zinazoonyesha kuwa gharama zake za kisheria zilifikia pauni milioni 34.5, sawa na takribani dola milioni 47.
Mzozo kuhusu ulinzi wa polisi
Harry pia amekuwa katika mzozo wa kisheria na serikali ya Uingereza kuhusu ulinzi wa polisi anapokuwa nchini humo.
Prince huyo amesisitiza kuwa yeye na familia yake wanahitaji ulinzi wa polisi wenye silaha kwa sababu wanakabiliwa na hatari kutokana na hadhi yao kama wanafamilia wa kifalme, hata kama hawana majukumu rasmi ya kifalme.
Baada ya kushindwa katika kesi kuhusu suala hilo mwaka uliopita, Harry alisema alikuwa tayari kujenga upya uhusiano wake na familia.
“Ningependa sana kupatana na familia yangu. Hakuna maana ya kuendelea kupigana,” Harry aliambia BBC. “Sijui baba yangu amebakiwa na muda gani.”
Ziara ya hivi karibuni ya Uingereza
Hatua ya kwanza kuelekea maridhiano ilionekana mwezi uliopita, wakati Harry aliporejea Uingereza kwa shughuli kadhaa za hisani.
Meghan na watoto wao walijiunga naye kwa sehemu ya ziara hiyo, ambapo walipata nafasi ya kutumia muda na King Charles katika makazi yake ya Highgrove, magharibi mwa Uingereza.
Ilikuwa mara ya kwanza Archie na Lilibet kumuona babu yao tangu sherehe za miaka 70 ya utawala wa Queen Elizabeth II mwaka 2022.
Hata hivyo, licha ya Harry kukutana na baba yake, bado hakuna dalili kubwa za kuboreka kwa uhusiano wake na kaka yake, Prince William, ambaye ndiye mrithi wa kiti cha ufalme.
Peter Hunt, aliyewahi kuwa mwandishi wa masuala ya familia ya kifalme wa BBC, amesema kurejea kwa Harry nchini Uingereza kunaweza kumweka William katika mazingira magumu zaidi.
Kwa mujibu wa Hunt, kurejea kwa Harry kutampa nafasi zaidi ya kujenga upya uhusiano na baba yake, huku uwepo wake nchini Uingereza ukifanya iwe vigumu kwa William kuendelea kuepuka uwezekano wa maridhiano na kaka yake.