
Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dar es Salaam, leo Agosti 21, 2026 imemkuta na kesi ya kujibu Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu katika kesi ya uhaini inayomkabili.
Uamuzi huo umetolewa na kusomwa na kiongozi wa jopo la majaji watatu wanaosikiliza kesi hiyo, Jaji Dunstan Ndunguru, kwa niaba ya majaji wenzake.
Jaji Ndunguru amesema baada ya kupitia na kuzingatia ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka pamoja na hoja za mshtakiwa, mahakama imejiridhisha kuwa Lissu ana kesi ya kujibu.
Lissu anashtakiwa kwa kosa la uhaini kinyume na Kifungu cha 39(2)(d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu iliyorekebishwa mwaka 2023.
Kosa hilo linahusishwa na kauli alizotoa katika mkutano uliofanyika katika Ofisi za Makao Makuu ya Chadema jijini Dar es Salaam, Aprili 3, 2025, kuhusu msimamo wa chama hicho wa kutoshiriki Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 na nia ya kuzuia uchaguzi huo.
Katika shtaka hilo, Lissu anadaiwa kuwa akiwa raia wa Tanzania, kwa nia ya uchochezi, alishawishi umma kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, kwa kutoa kauli na maandishi yaliyolenga kumshinikiza kiongozi mkuu wa Serikali ya Tanzania.
Akisoma uamuzi huo, Jaji Ndunguru amesema katika hatua hii mahakama inapaswa kuangalia iwapo, kwa kuzingatia ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka, mshtakiwa anaweza kutiwa hatiani. Amesema mahakama haihitajiki katika hatua hiyo kuingia kwa undani katika kuchambua ushahidi au kutathmini kiwango cha kuaminika kwake.
Katika kufikia uamuzi huo, mahakama imezingatia viini vitatu vya kosa la uhaini ambavyo upande wa mashtaka ulipaswa kuvithibitisha.
Jaji Ndunguru amesema moja ya mambo yaliyozingatiwa ni utii wa mshtakiwa kwa Jamhuri. Kwa kuwa Lissu alikiri kuwa ni raia wa Tanzania, mahakama imeona kipengele hicho kimeungwa mkono na ushahidi uliowasilishwa.