×

Tundu Lissu Kuendelea Kujitetea Kesi ya Uhaini Leo Mahakamani

Shauri la uhaini namba 19605/2025 linalomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu, linaendelea leo Agosti 24, 2026 katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dar es Salaam.

Kesi hiyo inaendelea katika hatua ya ushahidi wa utetezi, mbele ya jopo la Majaji watatu wakiongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru.

Hatua hiyo ilianza Ijumaa, Agosti 21, baada ya Mahakama kumkuta Lissu ana kesi ya kujibu na kumpa nafasi ya kuanza kujitetea dhidi ya mashtaka yanayomkabili.

Lissu, ambaye ameamua kujitetea mwenyewe, alianza kutoa ushahidi wake siku hiyo na pia akawasilisha orodha ya mashahidi anaotarajia kuwaita mahakamani.

Miongoni mwa mashahidi aliowataja ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan; Makamu wa Rais mstaafu, Philip Isdor Mpango; pamoja na Waziri Mkuu mstaafu, Kassim Majaliwa.

Aidha, Lissu amewataja baadhi ya viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na viongozi wa CHADEMA, akiwemo Makamu Mwenyekiti John Heche, Katibu Mkuu John Mnyika, Naibu Katibu Mkuu Amani Golugwa na Brenda Rupia.

Leo, Lissu anatarajiwa kuendelea na ushahidi wake wa kujitetea kama shahidi wa kwanza. Baada ya kukamilisha ushahidi wake, mashahidi wengine wa upande wa utetezi wanatarajiwa kuanza kutoa ushahidi wao.

Hata hivyo, suala la kuwaita viongozi wa Serikali, wakiwemo Rais Samia Suluhu Hassan, limezua mvutano kati ya pande hizo mbili.

Upande wa mashtaka umepinga wito wa viongozi hao kufika mahakamani, ukieleza kuwa Jamhuri tayari imekamilisha ushahidi wake na kwamba si jambo la busara kumtaka Rais kufika mahakamani kutoa ushahidi katika kesi hiyo.

Kwa upande wake, Lissu amepinga hoja hiyo akisisitiza kuwa sheria inapaswa kutumika kwa kila mtu bila kujali cheo au nafasi yake.

Kesi hiyo inaendelea huku ikifuatiliwa kwa karibu kutokana na uzito wa mashtaka na majina ya viongozi wakuu wa Serikali yaliyotajwa kuwa sehemu ya mashahidi wa utetezi.

Leave a Comment