
Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, leo Jumatano, Agosti 26, 2026, amehitimisha sehemu ya kwanza ya ushahidi wake katika kesi ya uhaini inayomkabili Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dar es Salaam.
Lissu ametoa ushahidi wake mbele ya jopo la majaji watatu likiongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, akisaidiwa na Majaji James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde.
Katika ushahidi wake, Lissu ameelekeza sehemu kubwa ya maelezo yake katika kuichambua hoja na ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka, akidai kuwa kuna mapungufu ambayo, kwa mtazamo wake, yanashindwa kuthibitisha shtaka linalomkabili kwa kiwango kinachotakiwa kisheria.
Lissu amesema upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi 17 kati ya 30 waliokuwa wameorodheshwa awali, akiwemo maafisa wa polisi pamoja na mashahidi waliolindwa ambao utambulisho wao haukuwekwa wazi kwa umma.

Katika hatua nyingine ya ushahidi wake, Lissu amepinga uzito wa ushahidi wa baadhi ya mashahidi wa upande wa mashtaka, akidai kuwa baadhi yao walikuwa wamewahi kukamatwa na polisi na baadaye kuachiwa baada ya kukubali kutoa ushahidi dhidi yake.
Pia amerejea baadhi ya vielelezo vilivyowasilishwa mahakamani, akiwemo maelezo ya onyo ya baadhi ya mashahidi wa upande wa mashtaka, huku akisisitiza kuwa vielelezo hivyo vinapaswa kutumika katika kutathmini kama mashtaka dhidi yake yamethibitishwa.
Awali, katika siku zake za kwanza za kutoa ushahidi, Lissu alieleza historia yake ya muda mrefu katika harakati za demokrasia, utawala bora na mageuzi ya mfumo wa uchaguzi nchini Tanzania. Pia alikanusha kuwa alikuwa na nia ya kufanya uhaini kupitia kauli alizotoa katika mkutano wa CHADEMA wa Aprili 3, 2025, ambao ndio unaohusishwa na shtaka linalomkabili.
Baada ya Lissu kumaliza ushahidi wake mkuu, mwenendo wa kesi umeahirishwa kwa muda wa saa moja na nusu, huku ikitarajiwa kurejea saa 8:30 mchana kwa hatua inayofuata ya dodoso kutoka upande wa mashtaka.
Katika hatua hiyo, Lissu anatarajiwa kuhojiwa na mawakili wa upande wa mashtaka kuhusu ushahidi alioutoa katika utetezi wake. Endapo muda utaruhusu, mashahidi wengine wa upande wa utetezi wanaweza kuanza kutoa ushahidi wao.
Kesi hiyo ni Criminal Session Case No. 19605/2025, Jamhuri dhidi ya Tundu Lissu, na inaendelea mbele ya jopo la majaji watatu wa Mahakama Kuu ya Tanzania.