The House of Favourite Newspapers

Amunike, Samatta wakubali Mziki wa Misri

TAIFA Stars usiku wa kuamkia jana walionyesha kiwango bora mbele ya Misri na Kocha Mkuu wa Stars, Emmanuel Amunike amesema kilikuwa kipimo sahihi kwao na amegundua kitu cha kukifanyia kazi fasta.

 

Stars ipo nchini Misri ikijiandaa na michuano ya Kombe la Afrika ambapo usiku wa kuamkia jana Ijumaa walicheza mechi ya kirafiki na Misri ambapo walichapwa bao 1-0 kwenye Uwanja wa El Arab uliopo kwenye mji wa Alexandria.


Timu hiyo imeweka kambi yake ya wiki mbili nchini Misri ikijiandaa na michuano ile ya Mataifa ya Afrika ambayo inaanza Ijumaa ijayo ambapo Stars ipo kundi moja na Algeria, Senegal na Kenya.

 

Amunike alisema kuwa mchezo huo ulikuwa mzuri na amebaini upungufu na ataufanyia kazi kuelekea kwenye mechi dhidi ya Zimbabwe itayopigwa kesho Jumapili mjini Cairo, Misri.

 

“Kwanza tumepata uzoefu kwa kucheza na timu kubwa kama Misri yenye uzoefu na kupitia wao tumebaini upungufu wetu
uko wapi ili tuweze kuufanyia kazi kabla ya mechi yetu ya kirafiki. Kwenye mechi na Misri zaidi niliangalia jinsi gani timu ilicheza na kutengeneza nafasi,”alisema Amunike.

 

Naye nahodha wa Stars, Mbwana Samatta alisema: “Mechi hii dhidi ya Misri ndiyo maana ya maandalizi kwa sababu huwezi kufanya mazoezi tu wakati hujui makosa yako yapo wapi na tumecheza na Misri ni timu kubwa na ugumu ambao tuliupata kwao ndiyo ambao tutaupata kwenye mechi za mashindano.”

 

Kwa upande wa meneja wa timu hiyo, Danny Msangi alisema kuwa jana Ijumaa wachezaji walifanya mazoezi mepesi asubuhi na mchana walirejea tena Cairo kuendelea na maandalizi.

#LIVE: KUBWA KULIKO YA YANGA KINACHOENDELEA MUDA HUU

Comments are closed.