The House of Favourite Newspapers

BAADA YA KUMWAGANA NA DOGO JANJA…UWOYA NDOA TENA!

Staa wa Filamu Bongo, Irene Uwoya

STAA wa Filamu Bongo, Irene Uwoya anafunga ndoa tena, Risasi Jumamosi limenasa ishu na mwenyewe amefunguka ukweli.  Uwoya ambaye awali aliolewa na msakata kabumbu, Hamad Ndikumana ‘Kataut’ (amefariki dunia) na kuachika, sasa anataka kutesti kwa mara nyingine ladha ya ndoa.

CHANZO CHAFUNGUKA

Chanzo kililiambia Risasi Jumamosi juzi (Alhamisi) kuwa baada ya Uwoya hivi karibuni kumwagana na mpenzi aliyetajwa kufunga naye ndoa ya siri, msanii wa Bongo Fleva, Abdulaziz Chende ‘Dogo Janja’ anafunga ndoa nyingine mwezi ujao.

MWANDISHI: Mbona ni kama kimyakimya.

CHANZO: Kimyakimya kivipi mbona hadi kundi (la WhatsApp) la kushughulikia mipango ya sherehe limeshaundwa.

MWANDISHI: Usiniambie; anaolewa na nani?

CHANZO: Mmh! Hilo la kuolewa na nani mimi sijui ila we jua anaolewa.

MWANDISHI: Ni tarehe gani sasa?

CHANZO: Ni kati ya tarehe 12 hadi 20 mwezi ujao.

MSIKIE UWOYA

Baada ya kupata tetesi hizo, mwandishi wetu alilazimika kumtafuta Uwoya ili kujua ukweli wa jambo hilo ambapo mahojiano yalikuwa hivi:

Risasi Jumamosi: Hongera Irene.

Irene: Hongera ya nini?

Risasi Jumamosi: Nasikia unatarajia kufunga ndoa hivi karibuni.

Irene: (Anacheka kidogo).

Risasi Jumamosi: Mbona unacheka ni kweli unaolewa?

Irene: We’ ni rafiki yangu siwezi kukuficha, ni kweli natarajia kufunga ndoa hivi karibuni.

Risasi Jumamosi: Ndoa hiyo utafunga lini?

Irene: Itakuwa mwezi ujao kwa majaliwa ya Mungu.

Risasi Jumamosi: Mbona muda mchache, hakuna kadi za mchango?

Irene: Hakuna mchango wowote, mimi nitatoa kadi za mwaliko tu na si kitu kingine, yaani nawaalika wanywe, wale na wafurahi na mimi kwa siku yangu hiyo muhimu.

Risasi Jumamosi: Ndoa yako hiyo unatarajia kufunga kanisani au msikitini?

Irene: Kanisani.

Baada ya jibu hilo mwandishi wetu aliamua kupotezea swali tata la uvumi kwamba aliwahi kubadili dini ili aolewe na Dogo Janja na kumuuliza vitu vingine ili kukamilisha vizuri mahojiano.

MASWALI YAENDELEA

Risasi Jumamosi: Mashabiki zako wangependa kufahamu ni nani anatarajia kukuoa?

Irene: Nisamehe, siwezi kumtaja, wanga wengi wanaweza kufanya hata hii ndoa kuishia njiani.

Rasasi Jumamosi: Watu gani umepanga kuwaalika?

Irene: Watu wangu wa karibu napenda wawepo kwenye harusi.

Risasi Jumamosi: Hili nakuuliza swali la kizushi tu. Vipi huoni kama utamuumiza aliyekuwa mumeo? Namaanisha Dogo Janja.

Irene: Sasa nitamuumiza nini wakati mimi na yeye tulishamalizana siku nyingi, ana maisha yake na mimi nina maisha yangu jamani.

Risasi Jumamosi: Ok, lakini umepanga kumualika kwenye sherehe yako?

Irene: Akitaka.

MTARAJIWA ABAKI KUWA SIRI

Aidha, jitihada za kunasa jina la mwanaume anayemuoa staa huyo wa filamu kupitia vyanzo mbalimbali ziligonga mwamba. Hata hivyo, hivi karibuni Uwoya amekuwa akitajwa kuishi maisha ya ‘kula bata’ sehemu mbalimbali ikiwemo Dubai katika nchi za Falme za Kiarabu ambapo mwanaume anayempa jeuri ya fedha ndiye anayetajwa kumuoa.

 

Comments are closed.