The House of Favourite Newspapers

Beki Rayon: Yanga kwanza, Simba baadaye

WAKATI Simba ikiendelea kumfukuzia beki wa kati wa Klabu ya Rayon ya Rwanda, Abdul Rwatubyaye, mlinzi huyo mwenye tatuu kibao mwilini ameweka wazi kuwa angependa zaidi kucheza Yanga na siyo Msimbazi.

Championi Jumamosi linafahamu kwamba, Yanga ambayo ndiyo ilikuwa timu ya kwanza Bongo kufanya mazungumzo na mlinzi huyo, waliambiwa watoe dola 60,000 (Sh mil 137) ili wampate, wakali hao kutoka Jangwani wakakubali.

 

Yanga imepanga kufanya usajili kwenye dirisha hili dogo lililofunguliwa Alhamisi iliyopita na litafungwa Desemba 15, mwaka huu huku kocha wake, Mwinyi Zahera akipanga mipango yote ya nafasi anazohitaji kwenye kikosi chake.

Rwatubyaye amezungumza na Championi Jumamosi moja kwa moja kutoka Rwanda na kusema kuwa, licha ya kumuachia nafasi kubwa meneja wake, Mupenzi Eto kusimamia mipango yake ya usajili lakini anatoa nafasi kubwa kwa Yanga kwa kuwa ndiyo walikuwa wa kwanza kumfuata na kuhitaji huduma yake.

Rwatubyaye aliongeza kuwa licha ya Simba kuwa bado hawajafika rasmi kwake kuzungumzia ishu ya usajili wake yeye anaona ni vyema kuipa nafasi kwanza Yanga kwa kuwa ilionyesha nia mapema zaidi.

“Yanga sina tatizo nao na hata ukiangalia awali hatukuwa tumefikia makubaliano mazuri kati yangu na wao lakini kwa kuwa meneja wangu ndiye anasimamia kila kitu naamini mambo yatakwenda vizuri kwa sababu naona kuna haja ya kutafuta changamoto sehemu nyingine.

 

“Nipo tayari kujiunga na Yanga kama wataweza kufikia makubaliano na meneja wangu pamoja na timu ambayo nacheza na siyo Simba ambayo bado hawajafika kwangu zaidi ya kuelezwa tu lakini nawapa nafasi Yanga kwa kuwa wao walikuwa wa kwanza kunifuata.

“Unajua wakati mwingine ubinadamu na busara vinahitajika kutumika kwenye kila jambo hapa washindwe wao tu,” alisema Rwatubyaye kijana mtanashati.

Ibrahim Mussa, Dar es Salaam

JESHI USU LA WANYAMAPORI LAZINDILIWA, SERENGETI MARA – VIDEO

Comments are closed.