The House of Favourite Newspapers

Bil 1.5 inawashusha hawa kiulainii Yanga

UONGOZI wa Yanga umepanga kumkabidhi Kocha Mkuu wa timu hiyo Mkongomani, Mwinyi Zahera kitita cha Shilingi Bilioni 1.5 kwa ajili ya usajili msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.

 

Fedha hizo atakabidhiwa kocha huyo Mei 18, mwaka huu kwenye Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam ambako kutakuwa na hafl a ya kuichangia timu hiyo. Kamati hiyo iliyokuwa chini ya mwenyekiti wake Naibu Waziri, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Anthony Mavunde ambayo imeahidi kukabidhi fedha hizo.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatano, uongozi hu mpya wa Yanga chini ya mwenyekiti wake msomi, Mshindo Msolla umepanga kukutana na kocha huyo mara baada ya mchezo wa jana dhidi ya Ruvu Shooting uliopigwa Uwanja wa Uhuru, Dar.

 

Katika kikao hicho, uongozi umepanga kupokea bajeti nzima ya usajili ya msimu mpya itakayowahusisha wachezaji wapya na wale wa zamani ambao mikataba yao inamalizika mwishoni mwa msimu huu.

 

Kitita hicho cha bilioni 1.5 kinatosha kabisa kufanya usajili bab kubwa kwa kuanzia na mshambuliaji wa Gor Mahia, Jacques Tuyisenge na beki wa kati wa AS Vita, Litombo Bangala wao wanataka dola 200,000 kila mmoja (zaidi ya Sh Mil. 460 kwa kila mmoja), Farouk Shikhalo ambaye kipa wa Bandari ya nchini Kenya yeye anataka Sh Mil. 80.

 

Kiungo mkabaji, Duke Abuya na kiungo mshambuliaji, Harrison Mwenda wote wanaoichezea Kariobang wanataka dola 25, 000 (zaidi ya Shilingi Milioni 50 kwa kila mmoja), Rodrick Mutuma anayecheza nafasi ya ushambuliaji anayeichezea Lupopo FC ya Congo yeye dau lake ni 40, 000 (zaidi ya Shilingi Milioni 90).

 

Wengine wapya ni wazawa ambao ni viungo washambuliaji, Hassan Kabunda, Charles Ilanfya wote wanaoichezea KMC, Kenny Ally (Singida United) na Ayoub Lyanga kila mmoja amewekewa dau la Shilingi 30 milioni.

 

Wanaotarajiwa kuongezewa mikataba ni Mkongomani, Papy Tshishimbi ambaye yeye msimu huu ametengewa Shilingi milioni 80 wengine ni Gadiel Michael, Mrisho Ngassa, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ ambao hao mikataba yao inamalizika mwishoni mwa msimu nao wamekewa dau la Shilingi Milioni 30 kila mmoja.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatano, Zahera amependekeza katika usajili wake wa wachezaji wazawa, dau la kila mmoja lisizidi Shilingi Milioni 30 ili kupunguza gharama za matumizi. Kwa hiyo kutokana na hali hiyo, usajili wa wachezaji wote hao wasipopunguza madau yao ya usajili Yanga italazimika kutumia Sh bilioni 1.6 ikiwa ni
ongezeko la Sh milioni 100.

 

“Kocha tayari amependekeza katika usajili wa wachezaji bajeti yao ni Shilingi Milioni 30 kwa wazawa pekee, kwani viwango vyao havitofautiani hivyo ni lazima wasajiliwe kwa dau hilo,”alisema mtoa taarifa huyo.

 

Kwa upande wa uongozi wa Yanga, Mwenyekiti Mkuu wa timu hiyo, Mshindo Msolla alisema: “Uongozi wetu umejipanga kusajili mchezaji yeyote atakayemuhitaji katika msimu ujao awe nje au ndani ya nchi, kikubwa tunataka kurejesha Yanga anga za kimataifa.

 

Wilbert Molandi, Sweetbert Lukonge na Musa Mateja

Comments are closed.