The House of Favourite Newspapers

Fei Toto Aletewa Jembe Jipya Yanga SC

YANGA msimu ujao haitaki utani ndiyo maana imeanza kufanya usajili wa kimyakimya kwa wachezaji kadhaa na sasa imefanya mazungumzo ya awali na kiungo wa Singida United, Kenny Ally wakitaka kumsaini akasaidiane na Feisal Salum ‘Fei Toto.’

 

Kenny Ally ambaye alikuwa akihusishwa kutua Yanga tangu dirisha dogo la usajili la msimu huu kabla ya kushindikana inadaiwa ni sehemu ya wachezaji ambao wamependekezwa na Kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera.

 

Championi linafahamu kuwa, uongozi wa Yanga umezungumza na kiungo huyo fundi wakimlainisha atue Jangwani kuongeza nguvu kwenye safu ya kiungo kwani imekuwa na upungufu kutokana na kuwategemea mastaa wawili tu, Feisal Salum ‘Fei Toto’ na Papy Tshishimbi.

 

Chanzo kimesema kuwa, juzi Alhamisi, Kenny alizungumza na mmoja kati viongozi hao wa Yanga kuhusiana na suala hilo na wanataka mambo yaende haraka ili kiungo huyo akapake mafuta sana eneo la katikati ya uwanja.

 

“Mazungumzo hayo yalienda vizuri na mchezaji alionyesha kuwa yupo tayari kujiunga na timu yetu kwa hiyo kilichobakia sasa ni jambo la sisi kumalizana naye, kwani kwa uwezo wake alionao naamini atatusaidia sana katika nafasi ya kiungo,” kilisema chanzo hicho.

 

Gazeti hili lilimsaka Kenny pia Kenny mwenyewe ambaye alifunguka kuwa: “Mkataba wangu na Singida unamalizika hivi karibuni baada ya ligi kuu, kwa hiyo hivi sasa naruhusiwa kufanya mazungumzo na timu yoyote ile.

 

“Kwa hiyo, kuhusiana na kuzungumza na viongozi wa Yanga siwezi kuweka wazi ila nipo tayari kujiunga na Yanga kama kweli wananihitaji na watakubaliana na mambo yangu ninayoyahitaji.”

Sweebert Lukonge, Dar es Salaam

KIKOSI cha YANGA Kilivyotua UWANJANI Kuivaa BIASHARA UTD

Comments are closed.