WAKATI kumejaa sintofahamu kuhusu Kocha wa Yanga Mzambia, George Lwandamina ambaye ametimkia kwao kujiunga na timu ya Zesco ya huko, kocha huyo anaweza kuwa msaliti wa Yanga.
Jinsi alivyoondoka Zesco wakati anakwenda kujiunga na Yanga, Kocha Lwandamina alifanya hivyo hivyo na sasa amerudia kitendo kile cha kuondoka Yanga kwa ‘gea’ ya kuwa anakwenda kwao Zambia kushughulikia mambo ya kifamilia huku tayari Klabu ya Zesco ya huko ikiwa imemtangaza kuwa atakuwa kocha wake tena.
Lwandamina anastahili kuitwa msaliti kwa maana anaiacha Yanga katika kipindi kigumu wakati inapambana kuwania kutetea ubingwa wake wa Ligi Kuu Bara, yeye anaondoka na pia katika wakati ambao Yanga ipo katika vita ya kupigania nafasi ya kwenda hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika.
Mtu wa namna hii ni sawa na askari anayekimbia vita, hivyo ni msaliti na hafai kabisa.
Yanga sasa inapambana angalau kuwania ubingwa mbele ya Simba na kutokuwepo kwake hata katika mchezo wa juzi Jumatano pengine imeweza kuwa sababu ya timu hiyo kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Singida United.
Lwandamina pia amekaririwa akitoa sababu nyingi huku akimlalamikia Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Boniface Mkwassa, lakini sababu zake hazina mashiko, bado yeye ni msaliti ambaye ameitosa meli baharini.
Anadai hakuwa akipata ushirikiano wa kutosha kutoka kwa Mkwassa, hili jambo alipaswa alizungumzie akiwa ndani ya timu na kitendo cha kwenda kuzungumzia kwao Zambia ni usaliti uliopitiliza.
Lakini Yanga wanapaswa pia wajifunze aina ya makocha kama Lwandamina, kama wao walitumia njia hizo na kumleta Dar es Salaam wakati wanaingia naye mkataba na yeye kuwadanganya Zesco yuko Dar es Salaam kwa shughuli zake binafsi, hiyo tu ilitoa picha kuwa Lwandamina ni mtu wa namna gani.
Ni msaliti na msaliti huwa haachi asili yake hapo ni sawa na jasiri kwani Jasiri Haachi Asili, sasa Lwandamina ameendeleza asili yake na Yanga inabidi wajutie kwa hilo.
Ingawa zipo hoja kuwa Lwandamina anadai mishahara yake na hajalipwa, njia aliyoitumia haikuwa kuitosa timu yenye mkataba naye na ilibidi akae na waajiri wake waone wanatatua vipi hilo na siyo kuondoka kihuni na baadaye kusikia anatangazwa kwenye timu nyingine.
Kwa sasa Yanga wanapaswa watulie wakati wanapolitatua suala hilo la Lwandamina vinginevyo watavurugika na kupoteza kila kitu.
Yanga inatakiwa kutafuta kocha ambaye ataendana na hali halisi ya klabu kwani kama hakuna fedha za kumlipa kocha wa gharama basi iache mpango wa kumpa kazi kocha wa kigeni badala yake ijikune pale unapoishia mkono wake.
Ila kwa hili alilofanya, Lwandamina hakwepi kabisa kuitwa msaliti na Yanga linapaswa kuwa funzo kwenu.
Lwandamina japokuwa naye ni binadamu mwenye mahitaji yake, lakini ameweka mbele maslahi binafsi kuliko hitaji la kazi yake kwani kama timu ingefanya vizuri basi malipo kwa wachezaji na benchi la ufundi yangekuwepo kama kawaida.
NA MAULID KITENGE
Comments are closed.