The House of Favourite Newspapers

Hans Poppe: Takukuru Wamenihoji Wakaniachia

0
Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe.

MWENYEKITI wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe amekiri kuitwa kisha kuhojiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru) ila hakushikiliwa kama ilivyoelezwa.

Juzi jioni baada ya Rais wa Simba, Evans Aveva na makamu wake Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ kupelekwa mahabusu kwa makosa nane ikiwemo kutakatisha fedha, uvumi ulizagaa kukamatwa kwa Hans Poppe pia.

Akizungumza na Championi Jumamosi, Hans Poppe alisema; “Kwanza nianze kwa kukiri kuwa niliitwa kuhojiwa na Takukuru, niliitikia wito kwa kwenda, nikahojiwa na baadaye nikaondoka.

“Siyo kwamba ninashikiliwa kama inavyotangazwa, kuhusiana na kuhojiwa tayari nilihojiwa kama mara mbili hivi kabla, hali hiyo ni ya kawaida ambayo inaweza kumtokea mtu yeyote.

“Ni kama ilivyotokea kwa rais na makamu wetu, waliitwa kuhojiwa lakini baadaye wakalepekwa

mahakamani kisha kupelekwa mahabusu, ila mimi sikupelekwa mahakamani walianiachia palepale.”

Aveva na Kaburu watafikishwa tena mahakamani Julai 13, mwaka huu kuendelea na kesi zinazowakabili mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Victoria Nongwa.

Wakati huohuo, Kamati ya Utendaji ya Simba inakutana leo Jumamosi katika kikao cha dharura ili kujadili mustakabali wa Aveva na Kaburu waliopo mahabusu.

Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba, Said Tully, alisema: “Sasa klabu inajiendesha bila ya kuwa na viongozi wake wawili wakubwa, hivyo tutakutana Jumamosi (leo) ili kupata watu watakaokaimu nafasi zao.”

Leave A Reply