The House of Favourite Newspapers

Kisa Simba, Yanga Yauza Jezi Kama Njugu

YANGA imezidi kuitangaza timu yao kimataifa, ni baada ya ndani ya siku nne kufanikiwa kuandika rekodi nzuri ya mauzo ya jezi yao, tangu wamefika kwenye Mji wa Ndola, Zambia.

 

Yanga wapo Zambia wakijiandaa na mchezo wa marudiano dhidi ya Zesco United ya nchini humo katika mchezo wa Raundi ya Kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Timu hizo leo zinatarajiwa kujitupa kwenye Uwanja wa Levy Mwanawasa, Zambia katika mchezo wa marudiano unaotarajiwa kujaa upinzani mkubwa kila timu ikitaka kuweka rekodi ya kufuzu makundi Afrika.

 

Yanga imepata nafasi ya kushiriki michuano hii msimu huu kutokana na Simba kufanya vyema kwenye michuano ya Caf msimu uliopita ambapo walifikia robo fainali hivyo Caf kuongeza timu kutoka mbili hadi nne, nyingine iliyopata nafasi ni KMC na Azam ambao ni mabingwa wa FA walikuwa na uhakika wa kushiriki kimataifa.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi, Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Frederick Mwakalebela alisema ushiriki wao katika michuano ya kimataifa, umekuwa na mafanikio makubwa nje ya nchi.

Mwakalebela alisema mafanikio waliyoyapata ni katika mauzo ya jezi zao rasmi za timu zinazouzwa na Kampuni ya GSM ambazo kwenye nchi mbili za Botswana walipokwenda kucheza na Rollers waliuza jezi 500.

 

Mauzo mengine waliyafanya Zambia ambapo leo wanatarajiwa kucheza na Zesco, tangu kufikia jana Ijumaa asubuhi waliuza jezi 420 na kufikisha jumla ya jezi 920 walizoziuza kwa nchi mbili.

“Kiukweli ushiriki wetu wa michuano hii ya kimataifa umetusaidia kuongezeka kwa mauzo ya jezi zetu rasmi za timu tangu tulipowapa tenda GSM waliyoishinda.

 

“Ni rekodi nzuri tuliyoiandika Yanga kwa muda mfupi katika mauzo ya jezi ambazo zimekuwa zikinunuliwa na mashabiki wetu wa Yanga waishio nchini hapo na maeneo ya karibu waliokuwa wakifika kuisapoti timu yao.

 

“Siyo kitu kidogo kwetu kuuza jezi 920 kwenye nchi mbili ambazo ni Botswana, tuliuza jezi 500 kabla ya hapa Zambia kuziuza 420 ambazo bado tunaendelea kuziuza kesho (leo) siku ya mechi yenyewe,” alisema Mwakalebela.

Wilbert Molandi, Dar es Salaam.

Comments are closed.