The House of Favourite Newspapers

Kocha Matola alia na TFF fainali FA

 

IKIWA imebakia siku moja timu za Azam FC na Lipuli FC ya Iringa kushuka dimbani katika fainali ya FA, Kocha Mkuu wa Lipuli FC, Selemani Matola ameonekana kuingia hofu katika mchezo huo kutokana na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutotaka kuwasikiliza malalamiko yao.

 

Lipuli FC itakutana na Azam FC kesho Jumamosi mkoani Lindi kwenye Uwanja wa Ilulu ikiwa ni siku chache baada ya kumaliza Ligi Kuu Bara msimu wa 2018/19.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Matola alisema kuwa wana wakati mgumu wa kuwafunga Azam FC kutokana na wachezaji wake kuchoka kutokana na kutumia muda mwingi safarini.

 

“Tunajipanga lakini ratiba inatubana mechi ya mwisho tumecheza Mbeya tumetumia siku mbili njiani hadi kufika Lindi, tunapata siku moja tu ya kupumzika, hivyo hatuwezi kufanya vyema.

 

“Tuliwaomba TFF watusogezee mbele mechi hiyo lakini imeshindikana na tumewaomba basi wasogeze nyuma mechi ya ligi imeshindikana kwa hiyo hatuna jinsi, tunajipanga kwa hali ilivyo kwani ratiba haipo vizuri.

 

“Kwa kweli sisi ni binadamu na si mashine ukizingatia tunasafiri siku mbili njiani kisha tunapewa siku moja tu ya kupumzika, siyo vizuri tulihitaji muda zaidi wa kupumzika hasa ukizingatia tunatumia usafiri wa basi, tunaenda kucheza tu hivyo hivyo,” alisema Matola.

Comments are closed.