The House of Favourite Newspapers

Konstebo Haruna Aguswa Na Mtandao Wa Polisi Wanawake Songwe

0

Kuelekea kilele cha siku ya wanawake duniani ambayo ni Machi 08 Mtandao wa Polisi wanawake Mkoa wa Songwe (TPF Net) wamemtembelea Askari mwenye matatizo ya kiuno na mgongo Konstebo wa Polisi Haruna wa kituo cha Polisi Ileje kwa ajili ya kumpa pole na kumkabidhi msaada wa vitu mbalimbali na pesa tasilim kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

Akizungumza baada ya kumkabidhi zawadi hizo Machi 06, 2024 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Theopista Mallya kwa niaba ya maofisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali amesema kuwa wameguswa na kuona umuhimu wa kurudi kidogo kilichopo kwa jamii na watu wenye uhitaji.

“Msaada huu umetokana na michango ya askari ambao walichanga na kununua zawadi hizo ili ziweze kuongeza pale kulipopungua kwa kipindi hiki cha muendelezo wa matibabu ya Askari Hamza” Alisema Kamanda Mallya.

Kwa upande wake, Konstebo Haruna amemshukuru Kamanda Mallya na Askari wote waliofika nyumbani hapo na amesema kitendo hicho kimemfariji na kumpa nguvu na kuona yupo pamoja na wenzake licha ya maradhi aliyonayo.

Jeshi la Polisi nchini limejiwekea utaratibu wa kuyatembelea makundi ya kijamii na watu wenye uhitaji kwa lengo la kutoa elimu na kutoa misaada mbalimbali ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii (Corporate Social Responsibility).

Leave A Reply