The House of Favourite Newspapers

Mama D nyodo 100%

ANATAAAMBA! Ndivyo unavyoweza kusema baada ya mama wa staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, Sanura Kassim ‘Mama D’ kuonekana akijiachia kwa nyodo asilimia mia na mumewe, Maisara Shamte ‘Anko’.  Tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia Jumatano wiki hii katika Viwanja vya Samaki- Samaki ndani ya Mlimani City jijini Dar ambapo kulikuwa na uzinduzi wa Albam ya Changes ya DJ wa Diamond, Romy Jones.

Wawili hao walionekana wakiingia katika viwanja hivyo na kwenda kuketi ambapo mama D, muda wote alionekana kuringa zaidi kwa kujibebisha mithili ya binti  aliyezama kwenye mapenzi. “Huyu si mama D jamani, ona anavyofanya na bebi wake yaani yale anayoyaonesha Instagram yamehamia hapa live sasa watu tunajionea wanavyojibebisha,” alisikika shabiki mmoja aliyehudhuria.

Hata baada ya kuitwa jukwaani, mama D aliongozana na Shamte wakishikana kimahaba na kuchukua kipaza sauti kwa mbwembwe kisha kuanza kumshushia sifa Rommy Jones huku akimzungumzia na Shamte. Mara baada ya kushuka, paparazi wetu alimsogelea mama D na kuanza kumhoji jinsi anavyojibebisha ukumbini hapo ambapo alijibu kwa nyodo.

“Acha nijibebishe maisha yenyewe ndiyo haya! Nawanyoosha vijana wadogo kwanza nina hadi cheti cha ndoa kama kuna mwingine  anabisha aje aoneshe cheti chake,” alisema mama D akionekana ‘maji’ yameanza kumzidi. Alipoulizwa pia kuhusiana na gari aina ya Toyota Land Cruiser V8 alilokabidhiwa na Diamond lina thamani gani alijibu; “Kwanza gari bado lipo ninalo, lina thamani ya shilingi milioni 200.”

Mama D ametokea kujizolea umaarufu kupitia mwanaye, Diamond. Amekuwa akijiachia na Shamte kwa kuweka picha tofauti mitandaoni wakionekana kimahaba huku akisindikiza kwa maneno ya vijembe. Hata hivyo, kuna madai kuwa amekuwa akijiachia kimahaba kuua soo la mwanaume wake huyo kudaiwa kuchepuka na kuzaa na mwanamke mwingine anayetajwa kwa jina moja la Sharifa.

Comments are closed.