The House of Favourite Newspapers

Manji Abadilisha Kambi Yanga

Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji

MAISHA yamebadi­lika ndani ya Yanga, ikiwa leo ni siku ya nne tu tangu Mwenyekiti Yusuf Manji arejee rasmi kwenye uongozi Jumapili iliyopita.

 

Manji ambaye ni mtaalam wa biashara, aliibuka Ju­mapili na kuzungumza na wachezaji ndani nya Uwanja wa Taifa na USM Algiers ikakumbana na kipigo cha mabao 2-1 katika mechi ya Shirikisho.

 

Championi Jumatano limejiridhisha kwamba tan­gu Manji aonekane ndani ya klabu hiyo mambo yame­kuwa safi ambapo timu imekuwa na hamasa ya kutosha hali inayowafanya hata wachezaji waliokuwa hawajitumi kuanza kuamka kwani wana matarajio ya neema kubwa.

 

“Tangu ajitokeze Mwenyekiti wetu Manji na kututia moyo siku ya mchezo wetu na Waarabu, kuna matumaini makubwa kwetu wachezaji kuwa nee­ma itashuka muda si mrefu kwani hadi leo hii timu ipo kambini inaonyesha wazi kuwa mkono wake ulishaingia katika kuisa­poti timu kwani mwanzo tulikuwa tukisuasua kwa mambo mengi likiwemo suala la kuchelewa kuingia kambini mapema tofauti na ilivyo sasa.

 

“Hata wachezaji wa­mechangamka, huku ndani ya kambi gumzo ni yeye tu hadi wachezaji wageni wameanza kuuliza kuwa jamaa ana nini mpaka kila mtu anapagawa,” kilisema chanzo chetu cha kuaminika ndani ya kambi ya Yanga.

 

“Maneno ya Manji muda mfupi kabla ya mchezo wetu na Waarabu yaliji­tosheleza sana kwetu kuona kuna jambo zuri linakuja kutoka kwake,” kiliongeza chanzo hicho.

Yanga imeweka kambi yake kwenye Hoteli ya Island iliyopo Manzese jijini Dar es Salaam na inaelezwa kuwa kila kitu kimekuwa kikienda sawa tofauti na mwanzoni.

 

Timu hiyo ilikuwa ikikabiliwa na ukata kutokana na kutokuwa na vyanzo vya fedha, lakini ujio wa Manji umewapa faraja kutokana na moyo wake wa kujitoa haswa pale panapokuwa na jambo la dharura la fedha.

Stori: Musa Mateja | Championi Jumatano

Comments are closed.