The House of Favourite Newspapers

Matola aibuka usajili Yanga

KOCHA msaidizi wa Lipuli FC ya Iringa, Selemani Matola amekiangalia kikosi cha Yanga na kutamka kuwa ni lazima wasajili washambuliaji, mabeki na kipa kama kweli wanataka kufanya vizuri kwenye msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.

Lakini akabainisha pia usajili wanaopaswa kufanya Simba ambayo ni timu yake ya zamani.

Matola ambaye ni mchezaji wa zamani wa Supersport ya Afrika Kusini, alisema, Yanga inahitajika kuwa na Makambo, Yondani mwingine wote wenye uwezo mkubwa kama waliokuwa nao katika timu hiyo katika kuelekea kwenye msimu ujao.

“Yanga inahitaji kuboreshwa kwa kuhakikisha wanazisuka safu mbili muhimu ambazo ni ya ulinzi ya kati na pembeni na ushambuliaji.

“Ukiangalia safu ya ushambuliaji akiwekewa ulinzi Makambo kama nilivyofanya mimi tulipocheza nao na kuwafunga, basi ni ngumu kwa timu hiyo kupata bao, ni ngumu kuwa na timu inayomtegemea mchezaji mmoja pekee,”alisema Matola.

Kuhusu Simba alisema; “ushauri wangu kwa Simba katika usajili ujao eneo la ulinzi lifanyiwe kazi zaidi sababu linahitaji umakini wa hali ya juu kama ni wachezaji hawa maproo walete wamaana ambao wataleta ushindani sio mchezaji aina kama ya Zana Coulibaly.

“ Ukiachana na ulinzi mbele wapo vizuri lakini wanahitaji pia mshambuliaji ambaye atawapa changamoto wale waliopo sasa na kuhakikisha wanapambana na kuibeba Simba.”

 

WILBERT MOLANDI | Dar es Salaam

Comments are closed.