The House of Favourite Newspapers

Mbasha Amvua Nguo Flora

0
Emmanuel Mbasha

 

BAADA ya mwanamuziki wa Nyimbo za Injili Bongo, Flora Mbasha kusambaza kitabu alichokipa jina la Siri za Flora Mbasha kilichoanika ‘mabaya’ ya aliyekuwa mumewe, Emmanuel Mbasha, mumewe huyo ameibuka na ‘kumchana’ vibaya mwimbaji huyo na kusema hafai kuwa mke.

 

Flora alikiachia kitabu hicho hivi karibuni ambapo pamoja na mambo mengine aliyopitia kwenye maisha yake na Mbasha, alieleza namna ambavyo mumewe huyo wa zamani alivyokuwa akimtesa na hata kumuingilia kwa nguvu akiwa kwenye siku zake.

Akizungumza na mwanahabari wetu katika ofisi za gazeti hili, Bamaga- Mwenge jijini Dar, Mbasha alianza kwa kueleza masikitiko yake juu ya kitabu hicho kwa kusema anashindwa kuelewa mume wa sasa wa Flora, Daud Kusekwa anajisikiaje pale Flora anapomzungumzia mara kwa mara.

“Yaani unajua watu wengine sijui wapoje bwana. Hivi kweli wewe hata huyo mwanaume wake anajisikiaje kuona mkewe ananiongelea kila wakati? Ni kukosa adabu, kwa nini wasifanye maisha yao?

Emmanuel Mbasha.

“Kweli mwanamke aliyefunzwa, akafunzika anaanzaje kumuongelea mwanaume wake wa zamani? Yaani kwangu mimi mwanamke wa aina hiyo anapoteza sifa ya kuwa mke,” alisema Mbasha.

Mbasha akizidi kutema cheche mbele ya kinasa sauti cha Amani, alisema kuwa, aliamua kukaa kimya baada ya kupitia mambo mazito na mwanamuziki huyo ambayo kamwe hataki kuyasikia wala kurudi nyuma.

“Ametaka talaka mahakamani, tumeachana na mimi sikutaka tena hata kumzungumzia, lakini yeye kutwa amekuwa akinizungumzia. Halafu kwanza unamzungumziaje mtu ambaye mlishaachana? Mtu ambaye kwanza hana hata habari na wewe, anafanya maisha yake mengine, huu kama siyo ujinga ni nini?” Alihoji Mbasha.

 

Kama hiyo haitoshi, Mbasha alizidi kumwaga mboga kwa kusema kuwa, siku zote sikio la kufa huwa halisikii dawa kwani kitendo anachokifanya Flora cha kumzungumzia yeye kama zilipendwa wake, alishakifanya kwake kwa mwanaume mwingine.

“Kifupi ni kwamba tabia ni kama ngozi, huwezi kuibadili. Wewe unaona sasa hivi anavyoelezea mambo aliyokuwa akiyafanya na mimi na kuongeza uongo wake, alishanifanyia hata mimi wakati nimemuoa.

Flora Mbasha

 

“Yaani yule mwanamke sijui bana, Mungu amsaidie. Yaani kwanza wakati mimi naanza kumfuatilia, huwezi kuamini, alikuwa na mwanaume mwingine. Akamuacha kwenye mataa wakati tayari walikuwa wanaelekea kwenye ndoa na vikao tayari walikuwa wameshaanza kufanya,” alisema Mbasha.

Mbasha ambaye kwa sasa hajaingia kwenye ndoa tangu aachane na Flora, alisema kuwa, anamshauri Flora aache kumzungumzia kwani kama ni ndoa ilishavunjika, aitazame zaidi ndoa yake mpya.

 

“Aachane na mimi. Namshauri atulie kwenye ndoa yake kuliko kila kukicha ni Mbasha… Mbasha…,” alisema Mbasha.

Mbasha na Flora walidumu kwenye ndoa kwa miaka 12 na kubarikiwa mtoto mmoja kabla ya kuachana mahakamani.

Kabla ya kuachana huko, Mbasha alituhumiwa kumbaka mdogo wa Flora na kesi kuunguruma muda mrefu na baadaye Mbasha alishinda hivyo kuachiwa huru.

 

 STORI: ERICK EVARIST | GAZETI LA AMANI |DAR

 

Ruge Mutahaba: Kama Makonda Hakutaka Nije Hapa Kwanini TEF Mliniita?

Leave A Reply