The House of Favourite Newspapers

Simba Mpya Hii Hapa

FRANCIS Kahata. Huyu ni yule mpishi wa mabao ya Gor Mahia ya Kenya na swahiba mkubwa wa Meddie Kagere anakuja Simba yaani muda wowote kuanzia wiki ijayo unaweza kuona picha lake la kutisha akitua pale Uwanja wa Ndege.

 

Siyo huyo tu, yule kiungo mwenye udambwidambwi uwanjani, Paul Were anayekipiga AFC Leopards ya Kenya naye amesema anakuja Simba. Huyo Were Orlando Pirates wanamnyatia na wao. Kahata ambaye alimng’arisha Kagere kwa kumtengenezea pasi na asisti za maana akiwa Gor Mahia, amewaambia viongozi wa klabu hiyo kwamba hataongeza mkataba anakwenda Simba.

 

Mchezaji huyo ambaye kwa sasa ndiye anambeba mkongwe Denis Oliech na Jacques Tuyisenge ndani ya Gor Mahia, mkataba wake unamalizika Julai na ameshindwa kuvumilia dau alilotajiwa na viongozi wa Simba kwenye simu walivyompigia siku mbili kabla ya mechi na Sevilla.

 

Habari ambazo Championi Jumamosi imejiridhisha nazo ndani ya Gor Mahia ni kwamba Kahata amewaambia viongozi wake kwamba Simba imemuahidi dau la uhamisho la Sh mil 60 na ushee pamoja na mshahara wa Sh. Mil 8.

 

Kahata ambaye timu yake iko kwenye wakati mgumu kiuchumi kwa sasa, habari zinasema Kagere amemshawishi kwamba atue Simba mambo ni mazuri kwelikweli na akamuelewa.

 

Lakini Mwenyekiti wa Gor Mahia, Ambrose Rachier alipoulizwa alikiri kusikia ishu ya Kahata na Simba lakini akawasisitiza kwamba waende wenyewe si kutumia mawakala kwani mchezaji huyo bado ana miezi saba kwao.

 

Pia habari zinasema kwamba hata Were ambaye ni mzaliwa wa Nyahururu, Kenya ni kati ya wachezaji ambao wanawindwa vikali na Simba na muda wowote wanasubiri simu za kutua Dar es Salaam kumaliza dili.

 

Kupitia mtandao maarufu wa mambo ya usajili wa Ujerumani, gharama ya usajili ya Were ni pauni 270,000 sawa na Sh mil 783 na ushee za Kibongo. Staa huyo mzoefu kisoka amewahi kucheza klabu za Amazulu ya Afrika Kusini, FC Kalloni na Kalamata FC za Ugiriki, mara ya mwisho alicheza Trikala FC ya Ugiriki kabla ya kujiunga na Zesco na baadaye AFC Leopards kwa mkataba mfupi.

 

Pia aliwahi kukipiga FC Kaiser ya Kazakhstan. Kiungo huyo mchezeshaji mwenye nguvu za miguu na mwepesi kunyumbulika, pia anamudu kucheza nafasi ya winga, mara nyingi amekuwa akitumia mguu wa kushoto na kuwachanganya mabeki wengi kutokana na chenga zake za maudhi na mashuti ya mbali.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi moja kwa moja kutoka Kenya, Were aliyezaliwa Oktoba 1993, alisema alipewa taarifa na wakala wake Oberta kutoka Ugiriki ambaye anasimamia mambo ya soka kutoka Ugiriki kuwa Simba wanamtaka.

 

“Simba hawajaja kwangu rasmi lakini wakala wangu ameniambia kuwa wananitaka na binafsi siwezi kukataa kama ofa itakuwa nzuri nakuja tu,” alisema Were mwenye uzito wa Kg 69. Mo amesisitiza kwamba wanasajili kikosi cha maana cha kushindana na klabu kubwa kama TP Mazembe, Al Ahly na Esperance.

Comments are closed.